Thursday, September 8, 2016

HATI ZENYE MASHAKA ZALALAMIKIWA MWANZA

SERIKALI imeshauriwa ‘kuwatumbua’ watumishi waliosababisha halmashauri za mkoa wa Mwanza kuendelea kupata hati zenye mashaka baada ya kutozingatia viwango vya kimataifa vya uandaaji wa hesabu (IPSAS).
Changamoto hiyo ilitolewa na baadhi ya wajumbe wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) wa Mwanza kilichofanyika jijini hapa wiki iliyopita, ambapo taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2014/2015 ilionesha kuwa halmashauri sita kati ya saba zinazounda mkoa huo zilipata hati zenye mashaka.
Halmashauri zilizopata hati zenye mashaka kutokana na ukaguzi huo wa CAG ni Jiji la Mwanza na wilaya za Kwimba, Magu, Misungwi, Sengerema na Ukerewe, huku Ilemela ikiwa ndiyo wilaya pekee iliyopata hati safi/inayoridhisha.
Taarifa hiyo ya CAG inataja makosa yaliyosababisha halmashauri hizo kupata hati zenye mashaka kuwa ni pamoja na watumishi husika kutozingatia viwango vya kimataifa vya uandaaji wa hesabu ambapo hazikuonesha thamani ya ardhi na viwanja vinavyomilikiwa katika hesabu za mwisho zinazoishia Juni 2015.
Sababu nyingine ni kufanya malipo ya fedha yenye nyaraka pungufu, kutowasilisha vitabu vya kukusanya mapato, kutopeleka fedha benki, kutoingiza madeni yanayodaiwa katika hesabu za mwisho na kutowasilishahati za malipo ya fedha.
Baadhi ya wajumbewa kikao hicho walielezea kukerwa kwao na makosa hayo ya kihesabu wakionesha wasiwasi kwamba huenda ni mpango wa makusudi uliosukwa na watumishi wachache kwa ajili ya kujinufaisha kiharamu na fedha za umma.
“Hali hii inatupa wasiwasi kwamba huenda ni namna ya watu fulani waliojipanga kuhujumu na kula fedha za umma kwa sababu haiwezekani halmashauri hizo sita kupata hati zenye mashaka kutokana na makosa yanayofanana.

“Inawezekana halmashauri hizo hazina wataalamu wa masuala ya usimamizi wa fedha na huenda serikali imeajiri vilaza wasiyo na taaluma inayotakiwa,” alilalamika mjumbe wa kikao hicho, Edward Mboje aliyejitambulisha kuwa ni Katibu wa UDP Mkoa wa Mwanza.
Hata hivyo, licha ya kauli hiyo ya Mboje kuungwa mkono na wajumbe wengine kadhaa, hakuna majibu wala ufafanuzi uliotolewa katika kikao hicho kilichoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella
CHANZO: RAIA MWEMA


Previous Page Next Page Home