Saturday, February 3, 2018

ZIARA YA MH. MANSOOR JIMBONI













TAREHE 01.02.2018

MBUNGE wa Jimbo la Kwimba mkoani Mwanza, Shanif Mansoor, amesema asilimia 80 ya vijiji jimboni hapa vipo mbioni kupata umeme.

Amesema miradi hiyo ya umeme wa Rea Vijijini, itapatikana kwa kipindi cha kuanzia sasa hadi kufikia mwaka 2020, ili kuwasaidia wananchi kupata maendeleo.

Mansoor aliyasema hayo juzi katika ziara yake ya kikazi jimboni hapa, na kwamba anahitaji kuwasaidia wananchi kupata maendeleo ya kisekta.

"Napenda kusema kazi tumeshaanza. Mwaka huu kuna mradi mkubwa sana wa umeme wa Rea Vijijini. Baadhi ya maeneo umeme haujafika....lakini tutapata umeme hadi Mwakilyambiti.

"Kwa hiyo anapambana kuhakikisha asilimia 80 ya vijiji vya Jimbo la Kwimba vinapata umeme wa Rea, ifikapo mwaka 2020," alisema Mbunge huyo wa Jimbo la Kwimba na kuongeza:

“Naomba sana ushirikiano wenu wananchi, ili tuijenge Kwimba na taifa kwa ujumla katika maendeleo ya kweli.”

Katika hatua nyingine, Mansoor aligawa majembe ya kilimo 18,000 yenye thamani ya zaidi ya sh. Milioni 200, ambapo karibu kila kaya itanufaika na vifaa hivyo.

Alisema lengo la kuwawezesha wananchi vifaa hivyo vya kilimo, ni kuwawezesha kuzalisha mazao ya chakula na biashara.

Alisema kuwa, licha ya kuahidi kutoa vifaa hivyo kwa wananchi lakini pia amelenga kuinua uchumi wa kila mwananchi kupitia kilimo, ndani ya
Jimbo la Kwimba.

"Sitaki mpate tabu wakati mbunge wenu nipo. Halmashauri yetu ya wilaya nayo nimeipatia mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa vyumba vitatu vya maabara, katika Shule ya Sekondari Bujiku Sakila.”

Aliipongeza pia Serikali kwa kujenga mradi wa maji jimboni Kwimba, unaogharimu zaidi ya sh. Milioni 576.

Kwa mujibu wa mh.Mansoor, mradi huo tayari umeshakamilika kwa kiwango cha
asilimia 80, ambapo umelenga kupunguza kama si kuondoa kabisa adha ya maji katika jimbo la kwimba.

“Mimi mwenyewe nataka kila kijiji kiwe na mradi wa maji safi na salama ya kunywa kutoka ziwa victoria,umeme na miundombinu rafiki pamoja na kutengeneza barabara za mitaa ya miji inayoendelea katika jimbo la kwimba.

“Nimechimba mabwawa na visima zaidi ya 35 vya maji kwa nguvu zangu. Lengo langu ni kuwasaidia wananchi walioniamini na kunipa kura za kishindo katika Uchaguzi Mkuu wa 2015,” alisema Mansoor.

Wakati huo huo, Mansoor amewakatia bima za afya viongozi wote wa Halmashauri za Kata wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jimbo la Kwimba.

Alisema kuwakatia kwake bima viongozi hao ni lengo la kutaka kuwasaidia, katika changamoto za masuala ya afya, hivyo anahitaji kuona jamii inatekeleza vema majukumu yake.

SOURCE: GSENGO BLOG

Sunday, October 2, 2016

PICHA ZA KIKAO CHA BARAZA LA MADIWANI HALMASHAURI YA KWIMBA NA SUMVE PAMOJA NA WADAU WA ULINZI NA USALAMA






















Kikao cha Baraza la Madiwani kwaajili ya kupitisha hesabu za Halmashauri ya Kwimba mkoani Mwanza pamoja na Kamati ya Ulinzi na usalama ya wilaya kimeketi Sept 28 mwaka huu wilayani humo.









Thursday, September 8, 2016

HATI ZENYE MASHAKA ZALALAMIKIWA MWANZA

SERIKALI imeshauriwa ‘kuwatumbua’ watumishi waliosababisha halmashauri za mkoa wa Mwanza kuendelea kupata hati zenye mashaka baada ya kutozingatia viwango vya kimataifa vya uandaaji wa hesabu (IPSAS).
Changamoto hiyo ilitolewa na baadhi ya wajumbe wa kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) wa Mwanza kilichofanyika jijini hapa wiki iliyopita, ambapo taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2014/2015 ilionesha kuwa halmashauri sita kati ya saba zinazounda mkoa huo zilipata hati zenye mashaka.
Halmashauri zilizopata hati zenye mashaka kutokana na ukaguzi huo wa CAG ni Jiji la Mwanza na wilaya za Kwimba, Magu, Misungwi, Sengerema na Ukerewe, huku Ilemela ikiwa ndiyo wilaya pekee iliyopata hati safi/inayoridhisha.
Taarifa hiyo ya CAG inataja makosa yaliyosababisha halmashauri hizo kupata hati zenye mashaka kuwa ni pamoja na watumishi husika kutozingatia viwango vya kimataifa vya uandaaji wa hesabu ambapo hazikuonesha thamani ya ardhi na viwanja vinavyomilikiwa katika hesabu za mwisho zinazoishia Juni 2015.
Sababu nyingine ni kufanya malipo ya fedha yenye nyaraka pungufu, kutowasilisha vitabu vya kukusanya mapato, kutopeleka fedha benki, kutoingiza madeni yanayodaiwa katika hesabu za mwisho na kutowasilishahati za malipo ya fedha.
Baadhi ya wajumbewa kikao hicho walielezea kukerwa kwao na makosa hayo ya kihesabu wakionesha wasiwasi kwamba huenda ni mpango wa makusudi uliosukwa na watumishi wachache kwa ajili ya kujinufaisha kiharamu na fedha za umma.
“Hali hii inatupa wasiwasi kwamba huenda ni namna ya watu fulani waliojipanga kuhujumu na kula fedha za umma kwa sababu haiwezekani halmashauri hizo sita kupata hati zenye mashaka kutokana na makosa yanayofanana.

“Inawezekana halmashauri hizo hazina wataalamu wa masuala ya usimamizi wa fedha na huenda serikali imeajiri vilaza wasiyo na taaluma inayotakiwa,” alilalamika mjumbe wa kikao hicho, Edward Mboje aliyejitambulisha kuwa ni Katibu wa UDP Mkoa wa Mwanza.
Hata hivyo, licha ya kauli hiyo ya Mboje kuungwa mkono na wajumbe wengine kadhaa, hakuna majibu wala ufafanuzi uliotolewa katika kikao hicho kilichoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella
CHANZO: RAIA MWEMA


Sunday, August 14, 2016

KWIMBA TUITAKAYO ITAPATIKANA KWA USHIRIKI MZURI WA WANANCHI NA VIONGOZI


(Hizi ni salamu zangu kwenu viongozi na wananchi wa Kwimba katika awamu hii ya HAPA KAZI TU)
BY NGUDU NYUMBANI BLOG
14/08/2016

Ni imani yangu kuwa wote tu wazima wa afya, tunaendelea na ujenzi wa taifa letu. Leo NGUDU NYUMBANI ingependa kuwakaribisha rasmi viongozi mbalimbali waliopewa majukumu mazito kuiongoza wilaya yetu kongwe ya KWIMBA katika awamu hii ya 5.
Bila shaka wengi wetu tunawafahamu viongozi wetu kuanzia ngazi ya vijiji, vitongoji, mitaa, kata, tarafa na hadi ngazi ya wilaya.

Kwa faida ya wengine ambao hawajui, Mkuu wa wilaya(DC) ya Kwimba kwa sasa ni  Mhandisi Mtemi Msafiri Simeon, Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya(DED) ni Pendo Anangisye Malabeja na Katibu tawala wa wilaya(DAS) ni  Andrea Izziga Ng’hwani. DED si mgeni kwetu sababu amewahi kuhudumu katika nafasi hiyo kabla.

Kuhusu wabunge wa majimbo ya Kwimba na Sumve bila shaka tunawajua, madiwani wetu na viongozi wengine wote wa ngazi zote tunawafahamu.

Awamu ya tano imeingia na kasi ya aina yake katika kuhakikisha inatoa majibu ya changamoto zinazowakabili wananchi wake, ikiongozwa vema na Rais wa JMT, Dr John Pombe Magufuli.

Katika mambo ambayo Rais  amekuwa akisisitiza kufanyiwa kazi na viongozi aliowateua katika ngazi mbalimbali hasa ngazi ya halmashauri za wilaya(mkurugenzi, Mkuu wa wilaya na Katibu tawala n.k) ni pamoja na;

Usuluhishaji wa migogoro ya ardhi  baina ya wakulima na wafugaji au wakulima dhidi ya mwekezaji au viongozi wa serikali na wananchi. Mfano mzuri ni mwezi wa pili mwaka huu pale Naibu waziri wa Ardhi, Nyumba na Maelndeleo ya Makazi Angelina Mabula alipombana Afisa ardhi wa wilaya ampatie maelezo kuhusu idara hiyo kuchukua fedha ya wananchi bila ya kuwagawia viwanja. Hayo na mengine mengi yanapaswa kupatiwa majawabu ya kudumu.

Tatizo la elimu hasa upungufu wa madawati ambalo kwa kiasi kikubwa limeshughulikiwa. Nilisoma taarifa moja ikimnukuu mkurugenzi wa wilaya akisema wilaya ya Kwimba ina nakisi ya madawati 5,314 sawa na asilimia 15 kumaliza tatizo la uhaba kufikia julai 30 mwaka huu. Hayo aliyazungumza wakati wa hafla fupi ya kupokea msaada wa madawati 60 yenye thamani ya Sh milioni 5 iliyofanyika shule ya msingi Kakora Kata ya Ngudu Mjini, kutoka kwa uongozi wa Benki ya CRDB tawi la Nyerere jijini Mwanza. Hivyo hadi kufikia julai 21 kulikuwa na upungufu wa madawati 5,254.

Maagizo mengine ya Rais ni pamoja na kukabiliana na baa la njaa pamoja na milipuko ya magonjwa katika mikoa na wilaya zote nchini.
Pia kupitia maagizo ya RC Mongella ya june 04 mwaka huu alipokuwa akiwaapisha  wakuu wa wilaya,  ambapo pamoja na yote alisisitiza wakasimamie shughuli za kuhimiza maendeleo, suala la ulinzi na usalama huku akitilia mkazo ukomeshwaji wa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi na vikongwe.

Katika kuwakaribisha huko NGUDU NYUMBANI ingependa kuwakumbusha machache yaliyopo ndani ya wilaya yetu.

ELIMU
Pamoja na kukabiliana na tatizo la madawati, zoezi lililofanikiwa kwa kiasi kikubwa. Wilaya yetu bado ipo nyuma sana katika suala la elimu. Ningependa kulielezea hili kwa kuhusianisha na matokeo ya vijana wetu kwenye shule za msingi na sekondari.
Bahati nzuri teknolojia imekua kiasi hata cha matokeo ya upimaji wa kitaifa darasa la nne(SFNA), Matokeo ya darasa la saba, ya kidato cha pili yote yanawekwa kwenye mtandao. Ukipitia blogu yetu utayaona na kukubaliana nami.

Tatizo ni kubwa sana katika ufaulu wa shule zetu, mathalani vijana wanaohitimu kidato cha nne. Niliandika makala yenye jina ‘IDADI YA WALIOCHAGULIWA KIDATO CHA TANO KWA KILA SHULE ZILIZOPO WILAYA YA KWIMBA’ pia NGUDU NYUMBANI ilifanya tathmini ya matokeo ya kidato cha 4 mwaka 2015. Kwa waliofuatilia matokeo kwa ujumla au walau kusoma tathmini wanaweza kukubaliana nami kuwa bado tuna safari ndefu katika elimu yetu.

Shule za A-level zilizopo wilaya ya Kwimba walau zinafanya vizuri katika matokeo yao. Ambapo katika matokeo ya mwaka huu,  Mwamashimba H/school wameshika nafasi ya 2/25 kimkoa(ina division 1-3, hakuna four na zero), Sumve ikishika nafasi ya 11/25 kimkoa na Ngudu H/school nafasi ya 12/25 Kimkoa.

Mbali na matokeo, bado sekta ya elimu ina changamoto lukuki, ikiwemo uhaba wa nyumba za walimu, madarasa, uhaba wa walimu n.k.  ‘Elimu ni walimu’ kauli hii imewahi kutolewa maelezo jadidi na mujarabu na Prof  Kitila Mkumbo katika moja ya makala zake kwenye gazeti la Raia mwema, pia wadau wengine wamepata kusisistiza kauli hii. Bila kuwekeza katika changamoto zinazowakabili waalimu bado elimu yetu itabaki nyuma daima dawamu.

Pamoja na yote hayo wilaya yetu inaburuza mkia katika ufaulu kimkoa kwa muda sasa. Hivyo viongozi wenye dhamana ya kusimamia sekta hii wasifanye kazi kwa mazoea tungependa kuona mabadiliko.

KILIMO NA HALI YA UCHUMI
MWANZA ni miongoni mwa mikoa(mitano) inayoongoza kwa umaskini Tanzania na asilimia ya umaskini(35.3 %) hii ni kulingana na mpango wa maendeleo wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/167.

kupitia gazeti la mwananchi waliandika kwamba, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dr, Tibeza alisema taarifa alizonazo zinatofautiana na alizopewa zinaonyesha kuwa Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa mikoa mitano inayokabiliwa na upungufu wa chakula.
Alinukuliwa akisema  “Taarifa nilizopewa na mthamini wa chakula zinasema Mwanza ni miongoni mwa (mikoa) inayokabiliwa na upungufu wa chakula, hivyo itakuwa na njaa, lakini wewe (Mongella-Mkuu wa Mkoa wa Mwanza) unaniambia kuna chakula cha kutosha,”.

Pamoja na yote hayo,asilimia kubwa ya wakazi wa Kwimba ni wakulima na wafugaji. wakulima  wanaotegemea zaidi mvua za masika ambazo mara nyingi hazieleweki na sio za kutegemea sana katika kilimo chao.

Mazao kama pamba, alizeti, mpunga, mahindi n.k ndiyo huliwa na wakulima japo ni kwa uchache ambao wengi wengi wao hulima kukidhi mahitaji ya familia na wachache hutegemea kuuza kujipatia kipato. 
Changamoto zilizopo hasa kwenye zao la pamba mikoa ya kanda ya ziwa ni nyingi na hazijapata ufumbuzi wa kudumu. Licha ya kuwa vinu kadhaa vya kuchambulia pamba bado zao hili halimnufaishi ipasavyo mkulima.

Bwawa la mahiga maalumu kwa kilimo cha umwagiliaji na uvuvi, kunapaswa kuwepo mipango mizuri katika kulitumia bwawa hili ili liweze kuwanufaisha wananchi na serikali kwa ujumla.
Elimu inapaswa kutolewa kwa wakulima, hasa kulima mazao yenye kuhimili ukame, utumiaji bora wa zana bora za kilimo n.k

UKUAJI WA TEKNOLOJIA
Ukuaji wa sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano kwa miaka ya hivi karibuni, imekuwa ikikua kwa kasi ukilinganisha na uhitaji wa watumiaji wa huduma zihusianazo na sekta hiyo. Kumekuwa na uwekezaji mkubwa katika hili, hali ambayo inatia moyo japo sio kwa kiwango kinachotakiwa lakini walau inaridhisha. 
Ukuaji wa TEHAMA umesababisha mabadiliko ya uendeshaji wa shughuli za serikali na jamii kwa ujumla.
Ukuaji wa sekta hii unahusisha na vitu vingi ambapo baadhi ni kama matumizi bora, sahihi na salama ya vifaa na mifumo ya TEHAMA  serikalini. Mbali na hilo pia, lengo jingine kubwa ni kurahisisha upatikanaji wa habari, uhuru wa kupata habari na kusambaza kwa wengine bila kuathiri, kuingilia, kukiuka au kuvunja katiba na sheria zote za nchi zinazolinda uhuru huo.  

Kwa leo nitaongelea zaidi kuhusu matumizi bora na sahihi ya vyombo vya Tehama hasa kwenye matumizi ya mitandao na intaneti(tovuti, barua pepe n.k)

Kuna uhitaji mkubwa kwa taasisi ama za serikali au binafsi kuwa na tovuti katika hatua mojawapo ya kurahisisha upatikanaji wa mambo muhimu yahusuyo taasisi husika. Hasa nikiongelea upande wa serikali, mamlaka zake nyingi zinatunza na kutoa taarifa zao kwenye tovuti. Ofisi ya Rais, na ofisi nyingine nyingi kubwa zinafanya hivyo pia.

Ni utaratibu mzuri unaokubalika katika kukuza secta ya TEHAMA, ambapo unarahisisha upatikanaji wa habari muhimu kwa wale wenye uwezo wa kutumia mitandao na intaneti kwa ujumla.
Ombi langu kwa hawa viongozi wetu ni kuhakikisha wilaya inakuwa na tovuti rasmi ambapo, habari zote muhimu za wilaya yetu zenye kupaswa kuwafikia wananchi ziweke kupatikana kule.

Sambamba na uanzishwaji wa hiyo tovuti, itasaidia viongozi waandamizi wa serikali ngazi ya wilaya kutumia barua pepe za serikali.

Mwongozo wa matumizi bora, sahihi na salama ya vifaa na mifumo ya Teknolojia ya habari na mawasiliano(TEHAMA) serikalini toleo la julai 2012, umesisitiza matumizi wa anwani za barua pepe hasa usajiri wa barua pepe za serikali.

 Anwani za barua pepe binafasi mfano  ‘yahoo.com’, ‘hotmail.com’, ‘gmail.com’ n.k hazipaswi kutumika katika mawasiliano ya shughuli za serikali.

Sasa sijui viongozi wetu wanatumia anwani zipi maana inaelekezwa taasisi za serikali anwani za barua pepe zao ziwe zenye kikoa cha mfumo wa ‘.go.tz’ na mfumo wa kifupisho cha cheo jina la taasisi na kikoa husika. Mfano anwani ya barua pepe ya mkurugenzi inaweza kuwa.. md@kwimbadc.go.tz na sio dedkwimba@yahoo.com iliyokuwa inatumika kabla.

Hiyo kwimbadc.go.tz  ndio tovuti inayopaswa iwepo hewani kwa maana ya kupatikana muda wote(umiliki wa domain name).

Kuna shida katika tovuti ya mkoa(www.mwanza.go.tz) hasa katika viungo(links) za wilaya, waliopata kutembelea tovuti hii wanaweza jua ninachomaanisha.

Mfano ukifungua kwenye link ya ‘Kwimba DC’ utafunguliwa ukurasa ukiwa wazi na ujumbe ukisema ‘Ukurasa huu upo kwenye matengenezo’  ni zaidi ya miaka miwili na zaidi sasa, enewei pengine matengenezo yanahitaji mwongo mzima tuendelee kusubiri.
Pamoja na hayo yote, kuna blogu moja(www.kwimbadc.blogspot.com) inayoripoti baadhi ya taarifa za halmashauri, japo sina hakika kama ndiyo inayotambulika. Kupitia blogu hiyo kuna ‘jarida la Kwimba’ toleo la 45 lenye jina ‘IJUE KWIMBA’.
 Kwa ambao hamjapata kusoma ni vema mkapitia kuna mambo mazuri ya kuyajua mule japo kwa ufupi. Pia kuna Documentary ya miaka 10 ya maendeleo ya KWIMBA 2005-2015.

Ningependa kumaliza kwa leo, kwa kunukuu baadhi ya maneno kwenye kitabu cha Uhuru na Maendeleo kilichoandikwa na Baba wa Taifa hayati Mwl J.K Nyerere, alisema;

Kama maendeleo yanaongeza uhuru wa watu, basi lazima yawe maendeleo yanayowafaidia watu. Lazima maendeleo hayo yawe na faida kwao, na kumaliza shida zao. kila mpango uamuliwe kwa kupima kama unatimiza shabaha ya maendeleo, na shabaha ya maendeleo ni  watu. Lakini kama mpango unasaidia maendeleo ya watu na kama unatimizwa na watu kwa hiari yao, mpango huo utatimiza haja za watu, mradi masharti matatu yametimizwa. Kwanza, kama watu wanaelewa shida zao. Pili, kama wanaelewa jinsi shida hizo zinavyoweza kumalizwa. Na tatu, kama wana uhuru wa kujiamulia mipango yao, na kuitimiza.

Itaendelea……

Tafakari!

nguduone@gmail.com

Friday, August 5, 2016

HALMASHAURI KWIMBA YAPOKEA MADAWATI 60 YA CRDB NYERERE JIJI LA MWANZA YATAKA WADAU WANANCHI KUCHANGIA ASLIMIA 15 ILIYOBAKI









 HALMASHAURI ya Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza, inahitaji madawati 5,314 sawa na asilimia 15 kukamilisha agizo la Rais Dk John Magufuli ifikapo Julai 30 mwaka huu.
Kauli hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Pendo Malebeja, wakati wa hafla fupi ya kupokea msaada wa madawati 60 yenye thamani ya Sh milioni 5 iliyofanyika shule ya msingi Kakora Kata ya Ngudu Mjini, kutoka kwa uongozi wa Benki ya CRDB tawi la Nyerere jijini Mwanza ikiwa ni kuunga jitiada za serikali ya awamu ya tano katika kuboresha miundombinu ya elimu nchini.
Malebeja alisema kwamba hadi juzi Halmashauri ilikuwa imetengeneza na kukarabati jumla ya madawati 30,006 sawa na asilimi 85 ambapo mahitaji halisi ni madawati 35,000 hivyo upungufu uliopo ni 5,314 sawa na asilimia 15 baada ya kupokea madawati 60 kutoka kwa wadau Benki ya CRDB upungufu sasa ni 5,254.
Akizungumza wakati wa kukabidhi msaada huo, Meneja wa CRDB tawi la Nyerere, Naomi Mwamfupe, alisema kwamba wao wanaunga mkono juhudi za serikali za kuboresha miundombinu ya Elimu, Afya, Mazingira, pamoja na kusaidi yanapotokea maafa na majanga lengo ikiwa ni kuleta usitawi wa jamii na kukuza uchumi.
“Tumewezesha wanafunzi 120 kukaa kwenye madawati baada ya wananchi wa Wilayah ii nao kujitokeza na kuchangia madawati kwa kushirikiana na serikali kwa asilimia 85 hivyo kwa mafanikio ya miaka 20 ya Benki ya CRDB nchini tunaunga mkono juhudi za Rais Dk Magufuli kuboresha miundombinu katika Sekta zote za utoaji huduma kuwa rafiki kwa wananchi,”alisema.
Mwamfupe alimtaka Mkurugenzi Malebeja na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Peter Ngassa (CCM), kufikisha ushauri kwenye Kikao cha Baraza la madiwani ili kuangalia uwezekano wa kufungua Akaunti katika tawi la benki hiyo lililopo ofisi za Halmashauri hiyo ili kuwapa fursa wadau mbalimbali na wananchi kujitokeza kwa hiali kuchangia maendeleo ikiwemo madawati.
Kwa upande wake mgeni rasmi aliyemuwakirisha Mkuu wa Wilaya hiyo, Katibu Tawala wa Wilaya (DAS), Andreaw Ng’hwani, alipongeza uongozi wa Benki hiyo tawi la Nyerere kwa kujitokeza kusaidia madawati ili kuwezesha Halmashauri kufikia lengo kwa asilimia 100 kama ilivyoagizwa na Rais Dk Magufuli nhini kote.  

 Chanzo: GSENGO BLOG

SENGA AZIKWA KIJIJINI KWAO KWIMBA

Waombolezaji wakilishusha jeneza lenye mwili wa marehemu Joseph Senga, aliyekuwa mpiga picha mkuu wa gazeti la Tanzania Daima, wakati wa mazishi yake yaliyofanyika kwenye Makaburi ya Kijijini kwao, Shushu wilayani Kwimba mkoani Mwanza





Mbunge wa jimbo la Sumve, Richard Ndasa akiweka shada la maua
Bi. Winfrida Senga akiweka shada la maua kwenye Kaburi la Mumewe, wakati wa mazishi yaliyofanyika kwenye Makaburi ya Kijijini kwao, Shushu Kwimba, Jijini Mwanza.
Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe akiweka shada la maua katika kaburi la aliyekuwa Mpigapicha Mkuu wa gazeti hili, marehemu Joseph Senga wakati wa mazishi yake yaliyofanyika katika Kijiji cha Shushi Wilaya ya Kwimba, Mwanza
MWILI wa aliyekuwa Mpigapicha Mkuu wa Gazeti la Tanzania Daima, Joseph Senga, ulipumzishwa katika makazi yake ya milele wilayani Kwimba mkoani Mwanza.
Senga (58) aliyefariki dunia Julai 27 mwaka huu nchini India, alizikwa nyumbani kwao katika Kijiji cha Shushi  wilayani Kwimba.
Maziko hayo yaliongozwa na Kiongozi wa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe ambaye pia mwenyekiti wa Chadema. Pia alikuwapo Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Vincent Mashinji  na   mamia ya waombolezaji.
Akizungumza katika maziko hayo, Mbowe alimuelezea Senga kuwa ni shujaa wa mapambano ya kupigania haki na demokrasia ya kweli nchini.
Alisema   kazi za  Senga aliyoiacha hapa duniani ni kielelezo thabiti cha uwajibikaji usioogopa vitisho.
“Senga alikuwa mfanyakazi na mtumishi mwenzetu. Senga hakuwa baraka kwa wana Kwimba pekee, bali alikuwa mtu wa wote. Nimefanya kazi naye kwa zaidi ya miaka 16. Tumezunguka naye kila eneo ndani ya nchi hii. Hakuna  operesheni ya Chadema tuliyomuacha Senga,” alisema Mbowe.
Vilevile, alisimulia mazingira tatanishi yaliyosababisha kifo cha aliyekuwa mwandishi wa habari wa Kituo cha Channel Ten mkoani Iringa, Daud Mwangosi.
Mbowe aliyetumia   dakika 20 kumzungumzia marehemu Senga, alisema usingekuwa ujasiri wake kupiga picha za tukio la kifo cha Mwangosi, dunia isingefahamu  polisi ndiyo waliohusika na mauaji hayo.
Senga ameacha mke mmoja na watoto saba, kati yao wanne wa kike na watatu wa kiume.
Mungu ailaze mahala pema peponi, roho ya marehemu,  Joseph Senga.

 Chanzo: MTANZANIA

Mpango wa Chandarua Kliniki wagawa vyandarua mkoani Mwanza.



Malaria yapungua mkoani mwanza 

Mpango wa ugawaji wa vyandarua unaojulikana kama CHANDARUA KILINIKI ulioanzishwa na serikali ya Marekani kupitia shirika la USAID umewafikia wananchi wa Mwanza mwishoni mwa wiki ikiwa lengo lake ni kuendeleza dhamira yake yakupambana na malaria nchini hasa kwa Mama wajawazito na watoto. 

Akitoa taarifa, wakati wa utambulisho wa mpango na ugawaji vyandarua kupitia kliniki ya wajawazito na watoto,Mratibu wa Malaria mkoa wa Mwanza Dk Saula Baichumila alisema Jumla ya wagonjwa 235 wa Malaria katika Mkoa wa Mwanza wamepoteza maisha kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu ambapo vifo 121 sawa na asilimia 51.5 ni vya watoto chini ya miaka mitano.

“Kutokana na vifo hivyo halmashauri ya Sengerema inaongoza kwa asilimia 27.6, Magu 20.4, Ukerwe 14.5, Nyamagana 11.9, Misungwi 11.1, Kwimba 8.5, Buchosa 3.4 na Ilemela 2.6,” alisema Dk Baichumila

Alisema mkoa umeendelea kupambana na ugonjwa huo kwa kushirikiana wadau mbalimbali ambapo kumekuwa na matokeo mazuri kwa ugonjwa huo kupungua hasa toka waliposhirikiana na USAID kupitia mpango wa CHANDARUA KLININKI mkoani Mwanza hadi sasa jumla ya vyandarua 142,360 tayari vimesambazwa kupitia vituo vya kutolea huduma za afya mkoani hapo.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella, Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Marry Onesmo, alisema maambukizi ya ugonjwa wa Malaria mkoani hapo yamepungua kutoka asilimia 19.1 ya mwaka 2011/12 hadi kufikia asilimia 15.1 mwaka2015/16.

Alisema lengo la mpango huo ni kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano vinavyosababishwa na malaria.Alisema takwimu za kitaifa za mwaka 2012 zinaonyesha kuwa kila vizazi hai 1000, watoto 54 hupoteza maisha huku malaria ikiongoza kuchangia vifo hivyo, huku kila vizazi hai 100,000 wajawazito 432 hupoteza maisha wakati wa kujifungua.

Mpango wa chandarua kliniki unatekelezwa na USAID chini ya mradi wa Vectorworks ambao ni mradi wa miaka mitano 2014-2019 ukiwa na dhumuni la kuongeza upatikanaji na matumizi ya vyandarua vyenye viatilifu vya muda mrefu kwa kushirikikiana na serikali ambapo wamejiweke lengo kuwa hadi kufikia mwaka 2016 kitaifa iwe imefikia asilimia 6 na mwaka 2020 iwe asilimia 1 kutoka asilimia 9 ya sasa.
Next Page Home