Sunday, November 29, 2015

TAARIFA KWA UMMA JUU YA KILIMO MKOA WA MWANZA.



JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
OFISI YA WAZIRI MKUU TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA

OFISI YA MKUU WA MKOA WA MWANZA TAARIFA KWA UMMA TAREHE 18/11/2015

Ndugu Wanahabari.
Mkoa wa Mwanza kwa kawaida hupata misimu miwili ya mvua kwa mwaka. Misimu hiyo ni ya mvua za vuli na masika ambapo mvua za vuli huanza kunyesha mwezi Septema/Oktoba hadi kufikia mwezi Januari; na msimu wa mvua za masika hunyesha Kuanzia mwezi Machi hadi Mei ya kila mwaka. Wastani wa mvua ni mm 720 hadi mm 1200 kwa mwaka ambazo hutawanyika kati ya mm 570 mm kwa mwaka hadi mm 1800 kwa mwaka.

Ndugu Wanahabari.
 Mkoa wa Mwanza unatarajiwa kupata mvua za wastani hadi juu ya wastani kwa maana ya mvua za juu ya wastani wa mm 1300 katika kipindi hicho cha Oktoba – Desemba, 2015. Hii ni kwa mujibu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).
Kwa kuzingatia utabiri huo wa hali ya hewa, tunawashauri wakulima na wananchi katika Mkoa wa Mwanza kufanya yafuatayo:-
Kulima mazao ya chakula aina ya wanga yanayohitaji au kustahimili mvua za wastani hadi mvua za juu ya wastani na pia kukomaa kwa muda mfupi kiasi cha kuweza kukomaa kufikia mwezi Desemba, 2015/Januari, 2016. Mkazo zaidi utiliwe kwenye mazao ya:-
Viazi vitamu hasa mbegu (Variety) zisizolikishwa (Non-Orange Fortified) aina ya Polista na Ukerewe, “Kishiga Mdege” na matembele; pamoja na mbegu zilizolikishwa (Orange Fortified) kama Ejumla, Karotoda na Kabode.
Mazao mengine ni mahindi hasa katika ukanda wa mazao (agro-ecological zone) unaopata mvua za wastani wa mm 1100 hadi 1200 kwa mwaka au Zaidi ukanda ambao unajumuisha Tarafa za Ukara na Ilangala katika Wilaya ya Ukerewe na Tarafa za Kahunda na Buchosa katika Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa. Aina ya mbegu (variety) za mahindi zinazopendekezwa ni:-
(i) Aina ya mbegu ya mahindi chotara (hybrid) ni pamoja na SeedCo yenye alama ya pundamilia (SC 513), Pannar inayokomaa kwa muda mfupi (PAN 4M-19) na kati PAN 15), Delkab (DKC 8053).
 (ii) Aina ya mbegu ya mahindi isiyochotara/ya chavua huria (OPV) ni pamoja na Kilima, Stuka, TAN 600H, Kitale na TMV 1. Mpunga hususan mbegu aina ya SARO 5 (TXD 306) na Supa inayolimwa mabondeni (low land rice); na NERICA 2 na 4 zinazolimwa nchi kavu.

Ndugu Wanahabari.
Tunawashauri wananchi wetu kutenga fedha na kununua pembejeo za kilimo hasa mbegu, mbolea na dawa za kilimo mapema kwa kuzingatia kuwa matumizi ya pembejeo yanaweza kuongezeka kutokana na mvua hizo ambazo zinaweza kusababisha kuoshwa ama dawa za kudhibiti wadudu waharibifu na magonjwa au mfumuko wa magonjwa hasa ya ukungu kutokana na mazingira ya unyevunyevu mwingi katika ardhi na hewani. Aidha, pembejeo zinaweza kupanda bei na kuwa adimu kutokana na kutopatikana kwa wingi na kwa urahisi kwa sababu ya mvua kuharibu miundombinu ya barabara hasa katika maeneo ya vijijini na kuathiri usafirishaji mazao. Ili kupunguza gharama za uzalishaji kutokana na mvua, wakulima wanaweza kugawanya kiasi cha mbolea kinanchohitajika kwa eneo na kuweka kwa awamu lakini pia tunawashauriwa kuwatumia Maafisa Ugani katika Wilaya.

Vilevile tunawashauri wakulima kulima kwa kukinga au kuzuia mmomonyoko wa udongo kutokana na mvua hasa katika maeneo yenye miinuko na vilima. Mmomonyoko wa udongo unaweza kukingwa au kuzuiliwa kwa kutumia mbinu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kulima kilimo cha matuta kwa kukinga/kukata mteremko, kulima na kuacha mistari (strip) ya nyasi au kufanya kilimo hifadhi. Zaidi, wakulima katika maeneo yanayo hifadhi unyevu kwa wingi au kutwaamisha maji (mabonde) wanaweza kulima kwa kufuata uelekeo wa maji kwa kuacha mistari ya nyasi kuzuia mmomonyoko wa udongo au kulima kilimo hifadhi kinachopunguza ukwatuaji wa udongo.

Ndugu wanahabari.
Tunawashauri wananchi kujiwekea akiba ya chakula hasa cha aina ya wanga kutokana na sababu kwamba mvua zinazotarajiwa katika kipindi hicho cha Oktoba na Desemba, 2015 zinaweza kuharibu miundombinu ya barabara na kusababisha ugumu wa usafirishaji wa vyakula hivyo kuleta uhaba wa vyakula katika masoko. Msisitizo wa kujiwekea akiba ya chakula unatolewa Zaidi kwa kuzingatia ukweli kwamba, Mkoa wa Mwanza wenye wakazi 2,772,509 huhitaji jumla ya Tani 708,376 za chakula aina ya wanga kwa mwaka mzima, ambapo, katika msimu wa kilimo wa 2014/2015 Mkoa ulizalisha Tani 495,863.2 za chakula aina ya wanga hivyo kuuwezesha kujitosheleza kwa 70% tu kwa chakula aina ya wanga.
Aidha, tunahimiza wafanyabishara kuleta chakula kutoka kwenye maeneo yenye ziada ya chakula aina ya wanga , lakini pia wananchi kutumia chakula kwa umakini na kuuza sehemu ya mazao ya biashara na mifugo ili kuweza kununua chakula. Aidha, Mkoa unasisitiza kuwa wafanyabiashara walioidhinishwa kununua na kuuza chakula kutoka katika maghala ya Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula Sumbawanga kufanya hivyo kwani mkoa umeutengewa jumla ya Tani 5,400 za mahindi kwa lengo la kuongeza upatikanaji wa nafaka katika masoko ya Mkoa wa Mwanza hii nikutokana na tathmini iliyofanywa na wadau.

Ndugu wanahabari
 Kupitia kwenu tunawaomba wananchi kujiwekea akiba ya chakula aina ya wanga katika ngazi ya kaya, kwa kuzingatia kuwa wastani wa watu katika kaya ya watu 6 katika mkoa wetu, tunawashauri kuhifadhi magunia 3 ya mahindi yenye uzito wa kilo 100 lakini pia magunia 5 ya muhogo mkavu yenye uzito wa kilo 60 kila moja sawa na kilo 314.64 katika kipindi cha Novemba 2015 na Januari 2016 endapo kaya hiyo itatumia mahindi au muhogo kama chakula cha wanga katika kipindi hicho.

 Kwa upande wa wakulima wanaotumia miundombinu ya umwagiliaji katika Skimu ya Umwagiliaji Mahiga kwenye Wilaya ya Kwimba tunawashauri kuchukua tahadhari kwani mabwawa yanaweza kukatika kutokana na mvua zinazotarajiwa na inaweza kusababisha mmomonyoko wa udongo, kusombwa mazao shambani, kukosa maji ya kumwagilia, kuongezeka kwa gharama za ukarabati wa mabwawa na hata kupoteza maisha ya watu na mali zao.

 Mwisho wakulima na wananchi kwa ujumla tunawashauri kuchukua tahadhari dhidi ya madhara yanayoweza kusababishwa na mvua zinazotarajiwa na kuzitumia vizuri mvua hizo katika kuzalisha mazao yanayopendekezwa ili Mkoa uzalishe chakula cha kuutosheleza katika msimu wa 2016/2017. Mara baada yakusema hayo niwashukuru sana kwakuja lakini zaidi sana kuweza kuchukua taarifa hii na kutufikishia kwa umma wa watanzania kupitia vyombo vyenu vya habari.

 Mungu Awabariki Sana , Ahsanteni kwa Kunisikiliza!


Chanzo:HAPA

Thursday, November 26, 2015

Hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, akifungua rasmi Bunge jipya la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dodoma, 20 Novemba 2015

Friday 20th November 2015

Mheshimiwa Spika;
Niko hapa leo kutimiza matakwa ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 91 Ibara ndogo ya kwanza inayonitaka kulihutubia na kulifungua rasmi Bunge hili. Naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya njema, na kutuwezesha kuwepo hapa siku ya leo. Aidha nitumie fursa hii kuwakumbuka wenzetu ambao, kwa namna na nafasi mbalimbali, walishiriki katika mchakato wa uchaguzi huu na kwa bahati mbaya walipoteza maisha yao kabla ya mchakato haujakamilika. Kwa hao wote waliotangulia mbele za haki ninamuomba Mwenyezi Mungu azirehemu roho zao na awape pumziko la amani. Nitumie nafasi hii kuwapa pole ndugu na jamaa ambao ndugu zao walifariki na wengine kupata ulemavu wakati wa mchakato wa uchaguzi huu.

Wednesday, November 25, 2015

HAWA NDIO WABUNGE 256 WALIOTHIBITISHWA NA TUME YA NEC


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Joseph Magufuli tayari ameapishwa na kuanza kazi… kwa upande wa Wabunge wenyewe bado.
Kinachosubiriwa ni kuitishwa kwa Bunge la 11 ambapo Spika Mteule pamoja na Wabunge wote wataapishwa… kingine kitakachofanyika ni uthibitisho wa jina la Waziri Mkuu, uchaguzi wa Naibu Spika na ufunguzi rasmi wa Bunge la 11.

Kulikuwa na stori nyingi sana wakati wa mchakato mzima wa Uchaguzi Mkuu ikiwemo matokeo kukataliwa na baadhi ya Wagombea, kwingine Uchaguzi haukufanyika kabisa, kwingine uchaguzi ulisogezwa mbele kwa sababu mbalimbali. Lakini mpaka leo November 12 2015 hapa ninayo majina ya Wabunge 256 ambayoTume ya Uchaguzi NEC imeyathibitisha kwamba wamepita kwenye Uchaguzi.

ILIKUWA NI LAZIMA MH MANSOOR ASHINDE UBUNGE JIMBO LA KWIMBA 2015


KOMANYA, BONIPHACE, mwandishi wa makala na mmiliki wa blogu
BY NGUDU NYUMBANI BLOG

Ni ukweli usiopingika kuwa, jimbo la Kwimba tangu mfumo wa vyama vingi kuasisiwa mwaka 1992,  na uchaguzi wa kwanza ukihusisha mfumo huo limeongozwa na chama tawala(CCM) kuanzia ngazi za serikali za mitaa, wawakilishi kama madiwani, mbunge, pia halmashauli kuwa chini ya usimamizi wa Ccm. Hali hiyo imeendelea kuonekana katika chaguzi zote zilizofuata nikimaanisha 2000,2005,2010 na 2015.
Japo kwenye uchaguzi wa wawakilishi serikali za mtaa mwishoni mwa mwaka jana wapinzani walipata uwakilishi kwenye baadhi ya vijiji na vitongoji japo haikubadili upepo kisiasa katika jimbo hili.

Kuna baadhi ya mambo au sababu zinazonipelekea kusema ndugu Mansoor alikuwa na nafasi kubwa kushinda ubunge jimbo la kwimba. Machache kati ya mengi ni kama ifuatavyo..

Moja, kukubalika sana maeneo mengi hasa vijijini. Hii ni kete kubwa kwa mgombea yeyote kuweka mazingira ya kushinda uchaguzi hasa ukizingatia vijijini ndio kuna mwitikio mkubwa wa wapiga kura. Imani hiyo kaijenga tangu agombee awamu iliyopita. Pia wananchi wengi walipata kumwamini katika miaka mitano iliyopita, kwa maana hiyo imani yao kubwa ilimjenga na kumpa imani kubwa ya kushinda awamu nyingine. Hapa namaanisha muitikio wao hasa kwenye kampeni zake.

Pili, nguvu ya pesa aliyonayo. Pia katika hili mgombea huyu alikuwa vizuri ukilinganisha na wapinzani wake. Katumia njia hii kucheza na akili za wananchi kwa kugawa kiasi cha fedha, nguo na vifaa vya chama. Pia katika hatua nyingine kupitia wapambe wake amegawa majembe baadhi ya vijiji kuhamasisha maendeleo. Njia hii imeongeza imani kwa wana ccm na wananchi wasio na vyama hata baadhi ya wapinzani wasio na msimamo kuwa na matumaini nae. Japo uhalisia ni kwamba inakosekana elimu ya uraia kwa wananchi kujua zawadi hizi kipindi cha kampeni hazina manufaa ya kudumu katika maisha yao ya kila siku ukizingatia hutolewa mara moja kila baada ya miaka mitano.

Tatu, kukosekana kwa upinzani imara wenye kuweza kujenga hoja na kuja na sera za kuweza kuwashawishi wananchi wawachague. Katika hili pia UKAWA kushindwa kufikia makubaliano ya kusimamisha mgombea mmoja na badala yake kusimamisha wawili ndugu Mh shilogela(CDM) na Mh Ntiga Otto(CUF) kulisaidia kwa kiasi kikubwa kugawana kura za upinzani na kumpa nafasi Mh mansoor kuwaacha kwa mbali kwenye mchuano.

Nne, kuwaaminisha wananchi baadhi ya mambo kama kayafanikisha. Kati hili ndugu Mansoor aliweza kuanisha mafanikio katika awamu iliyopita kama kuwaletea wananchi maji kutoka ziwa Victoria, umeme, kuwezesha ujengwaji wa  zahanati/vituo vya afya kadhaa. Kuweka mambo sawa ni kuwa kazi ya mbunge kwa mujibu wa katiba ni kuwakilisha wananchi, kutunga sheria na kusimamia serikali katika masuala ya maendeleo kama kusimamia miradi. Ila sio kweli kwamba kawaletea wananchi maji wala umeme, bali ni kupitia kuishauri na kuikumbusha serikali kufanya hayo na mengine jimboni kwake ila hana uwezo wa kutoa hela yake kufanikisha hayo. Katika hili la maji limekuwa likipigiwa kelele tangu kale na limekuwa likihubiliwa kwenye ilani ya ccm kila uchaguzi na limekuja kufanikishwa kwa kucheleweshwa kwenye uongozi wa JK japo lilikuwepo tangu enzi za Mkapa. Hapa naweza kuwapongeza Mh mansoor na Mh Leticia Nyerere ambao walipata kuliulizia utekelezaji wake kila walipopata nafasi kwenye bunge kuuliza swali au kujenga hoja kila mmoja katika nafasi yake. Katika hayo alifanikiwa kujipatia kura za kutosha.

Tano, jimbo bado ni ngome kuu(stronghood) ya chama tawala. Hili pia linachangia kwa asilimia kubwa kama sehemu ni ngome ya chama fulani miaka nenda rudi ni rahisi kwa chama husika kushinda japo kuna baadhi ya maeneo hali ilibadilika na ambaye hakutarajiwa kushinda.
Jimbo la Kwimba lipo chini ya Ccm kabla ya mfumo wa vyama vingi, baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama vingi hadi leo huku wakijikusanyia madiwani wengi na kuweza kuisimamia halmashauri. Kwahiyo upinzani walipaswa kutumia nguvu zaidi na njia mbadala za kuwawezesha kushinda.

MAONI YANGU
Nilipata kufatilia uchaguzi kwa kuwasikiliza wagombea kama Mh Mansoor, Mh shilogela na Ndugu Ntiga kusikiliza sera zao na hoja zao juu ya uwakilishi wa jimbo letu.
 Kiukweli nilimwelewa sana ndugu Ntiga Otto jinsi alivyokuwa akiwasilisha Mipango na mikakati yake juu ya kuiongoza Kwimba, japo ni hali isiyofichika kwamba ndiye alikuwa na wasikilizaji/wananchi wachache zaidi ukilinganisha na hao wenzake wawili waliokuwa na watu wengi.
 Hawa Iswalala(UDP) na mch. Yohana(ACT) sikupata kuwasikia ama kuhudhulia kampeni zao. Bila shaka kilichomwangusha huyu kijana aliyejimbanua(Otto) ni kutokukubaliana kwenye umoja wao. Pia ‘mind set’ za wananchi wengi ambao hawako tayari kusikiliza sera na kubakia kushabikia vyama zaidi.
Salamu zangu hizi zimfikie popote alipo na asikate tama ajipange kwa awamu ijayo.
Uchaguzi umeisha, mbunge na madiwani wamepatikana, cha msingi ni kuwapa support tuweze kufikia lengo la kupiga hatua ya maendeleo jimbo na wilaya yetu kwa ujumla.
 Malalamiko ya kwamba huyu mhindi, sijui sio mzawa hayatosaidia kitu zaidi ya kushirikiana na kiongozi aliyeshinda kusukuma gurudumu la maendeleo. Pia ideology ya kuwa mbunge ndio mtu sahihi wa kuleta maendeleo jimboni, ni ya kupuuzwa tu. kila mmoja wetu anayo nafasi ya kuleta maendeleo kwenye jamii yake na sio kusubiri fulani akuletee maendeleo mlangoni.
tunawa support viongozi wa ngazi zote tukiweka itikadi za vyama vyetu pembeni. Sote ni wamoja ubaguzi ni kuonesha udhaifu.

kutokana na machache niliyoyagusia hapo juu, nashawishika kusema kwamba Ilikuwa ni lazima kwa mh. Mansoor kushinda ubunge kwenye jimbo la Kwimba mwaka 2015.

KWIMBA TUITAKAYO
nguduone@gmail.com




Friday, November 13, 2015

TUME YATOA MAELEZO NA IDADI YA MADIWANI VITI MAALUM


JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UTEUZI WA MADIWANI WANAWAKE WA VITI MAALUM

Kwa mujibu wa Kifungu cha 86 A (8) cha Sheria ya Uchaguzi Serikali za Mitaa Sura ya 292, (Uchaguzi wa Madiwani) kikisomwa kwa pamoja na Vifungu vya 35 (1) (c) na 19 (1) (c) vya Sheria za Serikali za Mitaa (Tawala za Wilaya) na Na. 7 ya mwaka 1982 na Serikali za Mitaa (Tawala za Miji) Na. 8 ya mwaka 1982, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imepewa mamlaka ya kushughulikia na kutangaza Viti Maalum vya Madiwani Wanawake visivyopungua 1/3 ya Madiwani wa kuchaguliwa katika kila Halmashauri. Kwa kuwa Kata 3,957 zilifanya Uchaguzi Mkuu 2015 hivyo 1/3 yaViti Maalum vya Madiwani Wanawake ni 1,406. Hata hivyo, Tume haikuweza kugawa Viti vyote katika Halmashauri kutokana na kuahirishwa kwa Uchaguzi wa baadhi ya Kata katika baadhi ya Halmashauri nchini. Mgawanyo wa viti vilivyobaki utafanyika mara baada ya chaguzi zilizoahirishwa kufanyika.
Vyama vya Siasa vilivyoshiriki Uchaguzi Mkuu kwa upande wa Madiwani na kukidhi vigezo vya kisheria vya kupata Viti Maalum ni kama ifuatavyo:-


Jumla ya Viti vilivyogawanywa ni 1,392.
 Viti 14 vilivyosalia vitagawanywa mara baada ya Kata zilizoahirishiwa Uchaguzi kukamilisha zoezi la kupiga Kura
Majina ya Madiwani Wanawake wa Viti Maalum kwa kila Halmashauri walioteuliwa yataweza kupatikana kutoka Vyama na kwenye Halmashauri husika. Aidha tarehe 14/11/2015, Tume ya Taifa ya Uchaguzi itatangaza majina ya Madiwani wa Viti Maalum walioteuliwa. Ikumbukwe kuwa Tume imefanya uteuzi kwa kuzingatia Orodha iliyowasilishwa Tume na kila Chama kwa kuzingatia vipaumbele vya Chama husika.

Imetolewa na:
Jaji (Mst.) Damian Z. Lubuva
MWENYEKITI TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI

12/11/2015
Previous Page Next Page Home