Monday, May 23, 2016

STORI YA MAISHA YA NG'WANAMALUNDI-2

Bottom of Form
Chanzo: Mwananchi
Akiwa anaendelea na ngoma yake wananchi wa Kijiji cha Sekke waliibiwa ng’ombe wengi sana na watu kutoka Kabila la Wamasai ambao walienda kuwahifadhi katika Pori la Mwanima karibu na Kijiji cha Bubiki.
Ng’wanamalundi na kikosi chake waliondoka Wilaya ya Kwimba mkoani Mwanza na kuelekea Sekke wilayani Kishapu mkoani Shinyanga kwa lengo la kusaidia kuzikomboa ng’ombe zilizoibwa.
Hata hivyo kabla hawajafika uwanja wa vita, Ng’wanamalundi alifanya utabiri wake uliotokana na nguvu ambazo alizipata kutoka kwa Bibi Kizee wa porini.
Sitta anasema aliwaambia kuwa kabla ya vita, itatokea mvua kubwa sana na ikikatika watakuja ndege hai aina ya mwewe watakaokuwa wanazungukazunguka kwenye zile ng’ombe na hapo sasa wafuasi wake wakate miti mifupi mifupi (Lubugu).
Sitta anasema utabiri huo ulitimia, kwani mvua ilinyesha kubwa sana na baada ya kukatika wale mwewe walijitokeza wengi sana wakawa wanazunguka kwenye zile ng’ombe na ndipo yale mapigano ya Wamasai na wafuasi wake yalipoanza.
Aliwaeleza kuwa baada ya kuwa na fimbo ya Lubugu wale wenye upinde na mishale watakaa nyuma na kazi yao watakuwa wanazipiga zile ngao za Kimasai na zikidondoka chini ndipo wenye pinde na mishale waanze kushambulia.
Mwanamalundi alipigana hiyo vita ya Wamasai mpaka akazirejesha zile ng’ombe na aliwatokomeza Wamasai mpaka kwenye mpaka wa Mto Manonga unaotenganisha Tinde Shinyanga na Nzega mkoani Tabora.
Hapo ndipo ilibainika Wamasai hao walikuwa wametumwa kuiba ng’ombe Usukumani na Mtemi Tinginya wa Busongo Nzega, ambapo baada ya vita hiyo Ng’wanamalundi na kundi lake walirudi Sekke na kupewa jina la Kishosha Mang’ombe tafsiri ikiwa ni mrudisha ng’ombe.
Baada ya vita hiyo Ng’wanamalundi alirudi nyumbani kwao wilayani Kwimba kuoa, lakini bahati mbaya ilimkuta, kwani kila mke aliyejifungua, mtoto alikufa. Baba yake Bugomola akaenda Ntuzu kwa sasa Bariadi kufanyiwa tambiko kuhusu uzazi kwa mwanaye.
Akiwa huko Ntuzu, Bugomola alielezwa mwanaye Ng’wanamalundi hatapata mtoto kwa wake zake alionao. Hivyo aoe msichana atakayempata upande wa Mashariki ambaye atakuwa akiitwa Nkamba na atazaa watoto watatu; wa kwanza ataitwa Sitta, wa pili Ngassa na wa tatu Marieta.
Baada ya kurudi Bugomola, haikumchukua muda mwanaye Ng’wanamalundi akapata msichana akaoa na akaendelea na shughuli yake ya kuendesha kikundi cha ngoma.
Ng’wanamalundi kuwekwa kizuizini
Akiwa anaendelea na ngoma zake katika maeneo ya Kanda ya Ziwa, Sitta anasema siku moja yeye na kikundi chake walipokuwa wakiburudisha katika maeneo ya Bukumbi mkoani Mwanza, wafuasi wake walipumzika kwenye mti mkubwa ambapo pia kilikuwa Kituo cha Wajerumani, Ng’wanamalundi aliwaambia wafuasi wake waondoke waende kwenye ngoma, wafuasi wake waligoma wakadai wanapumzika kwenye kivuli hicho ili wavute sigara.
Baada ya kuwabembeleza vya kutosha akabaini hawataki kumsikiliza ndipo alipounyooshea kidole ule mti akisema “Ngh’walemelaga hanti gunugo aliyo gumaga,” akiwa na maana “Mmekatalia kwenye mti huo huku ukiwa umekauka.” Ghafla mti huo wote ulikauka.
Kuona hivyo wafuasi wake wakaondoka wote kwenye huo mti wakaenda kuendelea na ngoma yao ambayo walicheza katika eneo la Bukumbi na Busagara karibu na Mji wa Mwanza na walipomaliza walirejea Kwimba.
Akiwa Kwimba alicheza ngoma moja na Gindu Nkima, ngoma hiyo ilikuwa ngumu kwake ilichezwa sehemu za Mwanagwa. Baada ya kuwa amezidiwa Ng’wanamalundi, wapishi wake walimfuata na kumtaka awasaidie namna ya kupata kuni za kupikia.
Kutokana na uharaka aliokuwa nao Ng’wanamalundi alielekeza kidole chake kwenye miti ya minyaa iliyokuwa mbele yake huku akisema “Batemagi pye abenababa mkazugile,” akiwa na maana “Yakateni yote haya mkapikie.” Baada ya kauli hiyo minyaa yote ilikauka na kuwa kuni na wafuasi wake walikata wakaenda kupikia chakula.
Akiwa katika ngoma hiyo wakati huo barabara ya kutoka Shinyanga kwenda Mwanza ilikuwa inachongwa na manamba waliokuwa wakikamatwa na Wajerumani kwa ajili ya kazi hiyo, Gavana wa Kijerumani wa eneo la Mwanza alipita eneo hilo akiwa amepanda punda alikuta kazi imesimama, alipohoji kwanini kazi imesimama alielezwa wananchi wote wamekwenda kwenye ngoma ya Ng’wanamalundi.
Kitendo hicho kilimchukiza sana Mjerumani huyo, ambaye aliondoka akaenda Mwanza na baada ya siku mbili walikuja askari waliomkamata Ng’wanamalundi na kumfunga mnyororo na watuhumiwa wengine walipelekwa Mwanza na kuwekwa gerezani.
Kosa hilo kwa utawala wa Ujerumani lilihesabiwa kuwa ni uhaini wa kupinga utawala wao hivyo alitakiwa kupewa adhabu ya kunyongwa. Kabla hajapelekwa Mwanza, kwa kuwa ilikuwa ni safari ya kwenda kunyogwa, alipelekwa nyumbani kwa wazazi wake kuaga.
Alipofika nyumbani kwao alimpa mama yake shoka aliloliweka pembezoni mwa ukuta chumbani na maziwa, huku akitoa maelekezo.
“Mayu imbasa yeneye ulu yulina ng’wigulya mumhonatwalwa ulu yika hase mumhonashoka amabele genaya ulu guganda mumhonacha, ulu gita lububhi mumhonasata.” Akiwa na maana hii shoka ikipanda juu basi nitakuwa nimepelekwa ikishuka chini nitakuwa nimerudishwa.”
Sitta anasema Ng’wanamalundi aliendelea kumpa maelekezo mama yake kuwa haya maziwa yakiganda atakuwa amekufa na pindi yakipata utando atakuwa anaumwa, baada ya maelezo hayo Ng’wanamalundi alipelekwa Mwanza gerezani ambako alikutana na Mtemi Makongoro wa Mwanza.
Siku iliyofuata walitolewa wote ambapo Sitta alieleza kuwa walikutana pia na mganga aliyemtabiria kuzaa watoto watatu ambaye naye alikuwa amekamatwa kwa kosa la kupiga ramli iliyosababisha mauaji ya kishirikina.
Asubuhi kila mmoja alisomewa mashtaka yake ambapo Ng’wanamalundi alisomewa mashtaka matatu, shtaka la kwanza kuukausha mti uliokuwa ukitumiwa na maofisa wa utawala wa Wajerumani kama kituo cha kupumzikia huko Bukumbi Mwanza.
Shtaka la pili kuwatungia na kuwaimbia nyimbo mbaya Wajerumani na la tatu ni kukwamisha ujenzi wa Barabara ya Mwanza kwenda Shinyanga.

Ng’wanamalundi alidaiwa kuchezesha ngoma eneo la Mwanangwa hali iliyosababisha wafanyakazi wa manamba waliokuwa wakilima barabara hiyo kuacha na kwenda kuangalia ngoma yake hali iliyowachukiza Wajerumani…
Inaendelea...

STORI YA MAISHA YA NG'WANAMALUNDI-1


(Chanzo: gazeti la mwananchi, jan 2014)

Bottom of Form
Kwa Watanzania wenye umri mkubwa waliopata kusoma historia au kusikia hadithi za makabila, hasa ya Wasukuma na Wanyamwezi, hawakukosa kusikia habari ya Ng’wanamalundi.
Mtu huyo aliyewahi kuutingisha utawala wa Wajerumani, alizaliwa katika ukoo wa kawaida akiwa mcheza ngoma mashuhuri, mwaka wa kuzaliwa kwake haufahamiki ila alifariki dunia mwaka 1936, akiwa tayari mtu mzima.
Watu wengi wamekuwa wakimjadili kwa maoni tofauti, wengine wakimsifu kama shujaa huku wengine wakihusisha uwezo wake na nguvu za giza.
Katika makala hii usahihi wa historia yake unaelezwa na mjukuu wake wa pili, Kishosha Sitta (80) mkazi wa Kijiji cha Mwalugulu wilayani Kahama mkoani Shinyanga, anayesimulia alivyomfahamu babu yake huyo.
Sitta anaanza kueleza kuwa jina halisi la babu yake halikuwa Ng’wanamalundi bali lilikuwa Igulu Bugomola, ambaye alizaliwa katika Kijiji cha Mwakubunga Nera wilayani Kwimba mkoani Mwanza.
Ng’wanamalundi alikuwa mtoto pekee wa kiume na wa mwisho kati ya wanne, kwa baba yake Bugomola na mama yake, Ngolo Igulu.
Sitta anasema Igulu (Ng’wanamalundi), alikuwa na tabia ya uzururaji tangu utotoni na mara nyingi haikuwa rahisi kumkuta nyumbani. Alikuwa mashuhuri kutokana na umahiri wake wa kucheza ngoma na mara nyingi alipokuwa akitembea mitaani alifuatwa na kundi kubwa la watoto.
“Hali hiyo iliwachukiza wazazi wengi wenye watoto waliokuwa wakiambatana naye, kiasi cha kumchukia hata Ng’wanamalundi mwenyewe, kutokana na watoto wengi hasa waliokuwa wakitoka familia za wafugaji kutoweka na hiki kilikuwa chanzo cha mifugo mingi kupotea baada ya kutelekezwa na watoto hao,” anasema Sitta.
Hali ya kuchukiwa kwa Ng’wanamalundi ilienea pale kijijini kiasi cha kuanza kumkebehi, hasa kutokana na umbo lake refu na miguu yake myembamba kuanzia magotini hadi kwenye makanyagio, ikiwa mirefu kuliko kawaida.
Sitta anasema hali hiyo ilisababisha kumdhihaki na kumwongezea chuki zaidi kwa wanakijiji wa eneo hilo waliodiriki kumtukana kwa lugha ya Kisukuma; “Mamirundi galyo lilihumbura bana bise” ikiwa na maana ‘mamiguu yake marefu linarubuni watoto wetu”.
Hapo ndipo ukawa mwanzo wa kufutika kwa jina la Igulu na kuwa Ng’wanamalundi, jina ambalo lilitokana na urefu wa miguu yake na kila kona walimuita hivyo.
Kadiri siku zilivyosonga mbele Ng’wanamalundi alizidi kujiimarisha katika kikundi chake cha ngoma ambayo ilivuta vijana wengi, pia baadaye ilitumika kama jeshi la kukodiwa na Watemi inapotokea vita.
Pamoja na wazazi kumchukia sana, lakini vijana walimpenda na kikundi chake kikubwa cha ngoma kilipendwa na kutumika katika sherehe mbalimbali kwenye familia za Kitemi za wakati huo.
Mwanzo wa miujiza
Sitta anasema Ng’wanamalundi na wenzake wawili walikwenda kwa bibi kizee mmoja kutafuta dawa itakayowasaidia katika shughuli zao za kucheza ngoma, ambapo bibi kizee huyo alikubali kuwasaidia.
“Tujagi lolo ngh’wiporu bana bane akiwa na maana kwamba twendeni sasa porini watoto wangu. Mwanamalundi aliongozana na wenzake pamoja na kizee huyo mpaka porini.
“Walipofika porini bibi Kizee huyo alikamata vinyonga watatu na kuwaekea vichwani, kwa kila mmoja na kuendelea kusonga mbele porini, baada ya kufika katikati ya pori nene, kizee aliwaambia wote wasimame,” anasimulia Sitta.
Anasema baada ya kusimama aliamuru kila mmoja achimbe shimo lenye urefu hadi kiunoni, na baada ya kukamilika kwa mashimo hayo aliwaambia wakusanye kuni na kuzitumbukiza.
Baada ya kazi hiyo kukamilika Sitta anasema walipekecha moto na kuziwasha zile kuni na moto uliposhika kasi aliwachukua wale vinyonga watatu na kuwawekea dawa mdomoni na kisha aliwatupia ndani ya moto huo, wakateketea wote.
“Ng’wanamalundi na wenzake wakiwa bado wanashangaa vinyonga hao kuungua, ghafla alitokea kifaru kwenye moto huo na kuanza kuwakimbiza hovyo na wote wakasambaritika na bibi kizee wao,” anasema na kuongeza;
Ngw’anamalundi alikimbia akapanda juu ya mti, kifaru alifika kwenye shina la mti na kuanza kuliparua kwa hasira na baadaye aliondoka kabla hajafika mbali alimuona yule bibi kizee akikutana na faru huyo.”
Anasema Ng’wanamalundi alishuhudia kifaru akimrarua rarua bibi kizee mpaka akafa, kisha kifaru alitoweka kusikojulikana huku akimuacha Ng’wanamalundi asijue la kufanya juu ya mti.
Sitta anasema: “Ng’wanamalundi baada ya muda alishuka juu ya mti na kwenda kwenye maiti ya yule bibi kizee, akaamua aibebe mgongoni airejeshe nyumbani, lakini kabla hajafika mbali alisikia sauti ikisema, “Igulu bajahe abiyo akiwa na maana Igulu wenzako wamekwenda wapi”.
Sauti hiyo ilimshtua Ng’wanamalundi ambaye alimshusha bibi kizee mgongoni mwake na akashangaa kumuona akiwa hai asiyekuwa na jeraha lolote, kama alivyokuwa baada ya kushambuliwa na faru.
“Igulu tujage ahante ugo waliwalinaga, akiwa na maana Igulu twende kwenye mti uliokuwa umepanda, Ng’wanamalundi aliongozana na bibi kizee huyo mpaka kwenye ule mti aliyachukua magamba ya mti yaliyokuwa yameparuliwa na faru,” anasema Sitta.
Baada ya zoezi hilo kukamilika bibi kizee huyo alimtengenezea dawa aliyokuwa akihitaji, na kisha Mwanamalundi alirejea kwao kuendelea na shughuli zake za ngoma aina ya Kahena, ambayo mpaka leo inaendelea kwa jina lingine la Wigashe.
Anakutana na Mtemi Chlya
Sitta anaongeza kuwa, Ng’wanamalundi akiwa katika harakati zake za kujiimarisha katika masuala ya dawa zake za ngoma, alienda kuchimba kwenye pori la Mwandutu huko wilayani Maswa sasa ni Wilaya ya Kishapu, ambalo lilikuwa katika miliki ya Mtemi Chalya.
Imeelezwa kuwa baada ya kufika katika pori hilo akiwa na wafuasi wake wakiendelea kuchimba dawa, ghafla alitokea Mtemi Chalya na kumuuliza; “Ubebe nani wakuwilaga kwiza ngh’wiporu lyane” akiwa na maana; “Wewe nani amekuambia kuja kwenye pori langu?”
Mwanamalundi alimjibu; “ Ubebe ulintemi wa banhu pye nu nene nding’wenekele wa maporu pyee.” Akiwa na maana “Wewe ni Mtemi wa watu wote na mimi ni mmiliki wa mapori yote”. Kauli hiyo ilimuudhi Mtemi Chalya.
Anasema, kufuatia kauli hiyo Mtemi Chalya aliita jeshi lake kwa lengo la kuja kumkamata, lakini walishangaa baada ya kufika katika eneo waliloelezwa na Mtemi wao kuwa Ng’wanamalundi anatakiwa kukamatwa na kuuawa, lakini walishindwa baada ya kukuta simba wengi sana.
Jeshi hilo na Mtemi ilibidi kukimbia kujiokoa kwani simba hao walianza kuwashambulia, wengine walitawanyika ovyo na baadhi yao wachache tu ndiyo walionusurika.
Lakini cha kushangaza walipofika walimkuta Ng’wanamalundi na wafuasi wake wakimalizia kula chakula nyumbani kwa Mtemi Chalya, ambaye hata yeye alichanganyikiwa na kushindwa kuongea lolote.
Sitta anasema, Ng’wanamalundi baada ya kumaliza kula chakula kwa Mtemi Chalya aliondoka na wafuasi wake na akapitia kwenye lile pori akachimba dawa zake na kuondoka kwenda kuendelea na maisha yake.
“Katika ngoma zake; Ng’wanamalundi alikuwa na tabia ya kuwatahadharisha mashabiki wake kuacha kwenda wakiwa wamejipaka dawa yoyote ile, anasema. Aliwaambia: “Bing’we akwiziza munho wibilaga bugota bosebose ulu kutora akotora henaha,ulo nsabo akupandika heneha.”
Kauli hiyo ilikuwa na maana nyie asije mtu amejipaka dawa yoyote hapa kama ni kuoa, ataoa hapahapa kama ni mali atapata hapahapa, hata hivyo kuna wale walipuuza kauli hiyo kwa kuja wamejipaka dawa kwa lengo la kujipima uwezo wa dawa zao. Lakini hawakufanikiwa na badala yake walikufa.

inaendelea sehemu ya pili.....

Sunday, May 8, 2016

MBUNGE RICHARD NDASSA NA JIMBO LA SUMVE


BY NGUDU NYUMBANI BLOG
08/05/2016

JIMBO la Sumve ni moja kati ya majimbo mawili yanayounda halmashauri ya wilaya ya Kwimba. Ambapo linaundwa na tarafa mbili kati ya tano zinazounda halmashauri ya wilaya yaani Ngulla na Ibindo.
Jimbo pia linaundwa na kata 15, vijiji 60 na vitongoji  397. Wilaya ya KWIMBA inayoundwa na majimbo mawili ya KWIMBA na SUMVE ina  kata 30, vijiji 119 na vitongoji 870.

Kulingana na takwimu zilizotolewa mwaka jana(2015) juu ya makadilio ya idadi ya wapiga kura, jimbo hili lilikuwa na  Idadi ya watu 203,166 huku idadi ya watu wenye miaka 18 na kuendelea ni  87,993. Kata ya Maligisu ikionekana kuwa na wakazi wengi(22,449) na kata ya Bugando ndiyo yenye wakazi wachache zaidi(7,746).  

NAFASI ALIZOSHIKA
Mheshimiwa Ndassa kapata kuwa mjumbe katika kamati kadhaa zakudumu za bunge. Baadhi ya nafasi alizopata kuwapo ni kama ifuatavyo;

Kwenye bunge hili(bunge la 11) alipata kuwa  mwenyekiti wa kamati za kudumu bungeni kwenye kamati ya Uwekezaji wa mitaji ya umma(PIC).
Baadae akavuliwa  uwenyekiti na kuhamishwa katika kamati nyingine. Pia ana kesi inayomkabili ya kuomba rushwa ya mil 30(yeye na wenzake watatu), hivyo ana shitaka mahakamani.
Mwaka 2015 alipata kuwa mwenyekiti wa kamati ya nishati na madini, baada ya aliyekuwepo ndugu Victor Mwambalaswa kujiuzulu nafasi hiyo.

Mwaka 2000 alipata kuwa kaimu mwenyekiti wa PAC. Ambapo baada ya sakata la aliyekuwa waziri wa  Nchi ofisi ya Rais utawala bora Dk Hans Kitine kutumia fedha za serikali kumtibia mke wake nje ya nchi kwa kiwango cha dola za kimarekani 63,000 kinyume na utaratibu , yeye na wenzake walisimamishwa(kwa muda kuhudhulia vikao vya bunge) kwa kutoa taarifa za uongo.

 Hii ilikuwa katika bunge la mwaka 2001/2002. Kupitia kamati ya bunge ya hesabu za serikali(PAC) ambayo mh Ndasa alikuwa kaimu mwenyekiti, kamati iliandika barua Wizara ya afya ikiiagiza wizara hiyo kumrudishia mke wa Kitine pesa ambazo alikuwa ameshalipa kiasi cha dola 15,000. Kamati ilidai kugundua kwamba, Mama kitine alikuwa kweli anaumwa na alitibiwa nje ya nchi kwa kufuata utaratibu.

Ni katika kipindi ambacho ndugu Membe akiwa balozi wa Canada,  alisimama bungeni kueleza kwamba alikuwa na ushahidi bayana kuhusu ufisadi uliofanywa na Dk Kitine kwa jina la matibabu ya mke wake.
Alipopewa nafasi Membe akamwaga nyaraka muhimu zilikuwa zinaonesha jinsi fedha zilivyotumwa kwenye akaunti binafasi ya mama Kitine badala ya kutumwa katika akaunti ya ubalozi. Membe akiwa balozi wa Canada ndiye aliyepewa jukumu la kuchunguza uhalali wa matibabu na malipo ya mama Kitine. Mwisho wa siku katika hospitali zote zilizodaiwa kumtibu mama Kitine hawakupata ushahidi wowote  kwamba aliwahi hata kufika huko achilia mbali kutibiwa.

Kufuatia kuthibitika kwa kashfa ya Dr Kitine, ilionekana wazi kwamba kamati ya Bunge ilikuwa imetumika kujaribu kumsafisha Dr Kitine na familia yake. Kwa sababu hii wajumbe watatu wa kamati hii walifungiwa miezi miwili kuhudhulia vikao vya Bunge. Wajumbe hao walikuwa ni Richard Ndasa, Dk. Amani kaborou na Dk. Kitine mwenyewe.
Richard Ndasa ndiye mbunge wa kwanza kuomba wajumbe wa bunge la katiba kuongezewa posho zao za kila siku kutoka laki 3 hadi laki 7, sababu kubwa ikiwa ni kupanda kwa gharama za maisha. Ambapo katika ongezeko hilo lingeweza kusaidia kumudu mahitaji yao muhimu, pia kulipa madereva na mahitaji mengine binafsi pindi wakiwa Dodoma muda wa siku 90. Hii ilikuwa mwaka 2014 kwenye bunge la katiba. Mwanzoni hoja hii ililenga kuwasaidia wajumbe wale 201 walioteuliwa na Rais lakini baadae waliozidi kuunga mkono hoja hiyo waliibeba kama hoja ya wajumbe wote iwahusu.
Kupitia wizara ya fedha, ilitolewa taarifa iliyowataka wote wanaoona posho za sasa hazitoshi ni bora wakafungasha virago na kuondoka.

HARAKATI ZA UCHAGUZI.

Mheshimiwa Richard Ndassa kawa mbunge wa jimbo la Sumve katika awamu tano sasa ikiwemo na awamu hii. Yaani 1995-2000, 2000-2005, 2005-2010, 2010-2015, na 2015- mpaka sasa. Hii ina maana kwamba kawa mbunge katika awamu ya tatu yote chini Mkapa, kawepo kwenye awamu ya nne yote  chini ya Kikwete, na sasa yupo kwenye awamu ya 5 chini ya JPM.

Kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015, jimbo la Sumve lilikuwa na wagombea wanne.  NG'HOLO MALIMI LUBATULA- CHADEMA;  SHADRACK BONIPHAS GWEGWE- ADA TADEA;  MCHELE RICHARD NTUNDURU- CUF na  NDASSA RICHARD MGANGA- CCM
Matokeo ya mwisho kwenye uchaguzi huo,  Richard Ndasa (CCM) kura 20,002, Mchele Richard(CUF) kura 14,966 na Ng’holo  Malimi(CDM) kura 6,535.
Hivyo mgombea wa CCM akashinda ubunge kwa mara nyingine tena.

Mwaka 2010 kwenye uchaguzi mkuu, Richard Ndasa (CCM) alipata kura 18,705, mpinzani wake wa karibu ndugu Julius Samamba alipata kura 16,729.

Kwa mtizamo wangu, nadhani huyu ni mojawapo ya wanasiasa bora wenye kujua kucheza na akili za wananchi vyema.  Pia mwenye ushawishi mkubwa mathalan, kwenye bunge letu la JMT ndiyo maana utaona kapata kuongoza kamati kadhaa za kudumu za bunge.
Ni mwanasiasa  bora pia kwa kuweza kushinda uchaguzi katika awamu tano mfululizo au kwa maneno mengine naweza sema ni mshindi tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa kwenye jimbo la Sumve.  Jimbo lake ni mojawapo ya ngome kuu ya chama tawala ambayo haijapata kuyumbishwa hata mara moja.
Kushinda kwake katika chaguzi ndiyo kunaipa nguvu CCM kushinda katika nafasi nyingine za uwakilishi kama madiwani na Rais  na hata kwenye chaguzi  za serikali za mitaa.

Katika awamu zote alizoshinda uchaguzi na chama kupata madiwani wengi ambao wanakipa chama nafasi ya kuongoza Halmashauri wakiungana na wale wa jimbo la KWIMBA ambalo ni ngome kuu ya chama tawala pia.

Lakini pia  katika upande wa pili, ni moja kati ya wanasiasa mizigo wasiofaa kuigwa kama kiongozi kwenye jamii.

Nasema hivi kwa maana kwamba, hawezi na kashindwa kusimamia majukumu na wajibu wake ipasavyo kwa wananchi waliomchagua.  Huwezi nishawishi  kwamba, umeongoza jimbo miaka 20 lakini bado kuna changamoto nyingi ambazo nyingine zingeweza kutatuliwa kwenye miaka mitano tu ya mwanzo.

 Leo mbunge anaahidi kushughulikia tatizo la madawati mashuleni na yupo hapo miaka 20 kabla. Ndiyo kusema changamoto ya madawati imekuwa  mpya kwake hapo kabla haikuwepo?
Nimetolea mfano wa changamoto ya madawati, japo kuna changamoto nyingi ambazo kwa mwakilishi wenye sifa ya kuwa kiongozi anazijua na anaweza ama kuzitatua au kuzitolea ufafanuzi na ufumbuzi kwa kushirikiana na wananchi kuzipunguza na hatimaye kuzimaliza kabisa.
Na katika mambo yanayosababisha jimbo la Sumve na wilaya ya KWIMBA kubaki nyuma katika suala zima la maendeleo ukilinganisha na sehemu nyingine  ni uzembe wa ‘chama tawala’. Chama kilichopewa dhamana ya kuongoza jimbo,  halmashauri na serikali kwa ujumla. Ambapo wawakilishi wameshindwa  kutekeleza  wajibu wao ipasavyo wa kusimamia utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika jamii yetu.

Changamoto na/au matatizo mengi yaliyopo kwenye jimbo hili  mengi ni yaleyale kama yaliyopo kwenye jimbo la Kwimba. Na chama tawala ndiyo kimeongoza majimbo haya kwa miaka yote mpaka sasa. Nilipata kuelezea baadhi nilipoongelea jimbo la Kwimba huko nyuma.
Mimi kama mwananchi wa kawaida nitapenda ama chama tawala kisifanye mambo kwa mazoea(hasa kupitisha makada wachovu) na kikubali mabadiliko ndani ya chama. Kuna watu wengi wazuri ndani ya chama ila wanakwama kwa sababu hawana rasilimali(fedha, na watu) ili kuweza kuaminiwa na chama.

 Pia nitafurahi kama upinzani utajiimalisha vizuri kiasi cha kusimamisha watu makini awamu nyingine ili kutoa ushindani mkubwa na ikiwezekana kukiondoa chama tawala katika majimbo haya kama kitaendelea na uzembe. Lengo letu sote ni kuona jamii inasonga mbele kimaendeleo na sio vinginevyo.

NAFASI YA UPINZANI.

Wapinzani katika jimbo hili wangeweza kuwa na nafasi kubwa ya kuchukua jimbo hili tangu mwaka 2010 kama wangeweza kuungana na kuonesha ari na nia ya dhati ya kutaka kumwondoa ndugu Ndasa. Unaweza kuona katika matokeo ya mwaka huo, tofauti ya kura za Ndasa na mpinzani wake ndugu Samamba ilikuwa ni kura tu 1976 katika kura zaidi ya elfu 35 zilizopigwa. Hapo hatujahesabu kura za wagombea wengine ambao pengine wangeweza kumuunga mkono ndugu Samamba na upepo ungebadilika.

Uchaguzi wa mwaka 2015 pia hali haikuwa tofauti sana, kwamba kura za wapinzani wake ambazo zilikuwa ni 21,501(CDM na CUF) dhidi ya kura 20,002 za ndugu Ndasa. Kama wangeungana(kama makubaliano yao ya awali) basi ungekuwa mwisho wa utawala wa ndugu Ndasa katika jimbo hilo.

Inasemekana upinzani hasa wale wanaounda UKAWA walikubaliana  kuachiana jimbo hili ili asimame mgombea mmoja kati ya vyama hivyo, vyama vingine vimuunge mkono. Lakini hawakuweza kukubaliana na kufikia hatua hiyo ya kila chama kusimamisha mgombea. Hatua hiyo ilimrahisishia kazi mgombea wa Ccm na hatimaye kuibuka kidedea. 
Uzembe huu ulifanyika hata jimbo la Kwimba na majimbo mengine mengi ambayo kama upinzani ungeungana vema basi chama tawala kingepoteza majimbo zaidi ya ilivyo sasa.

Kama wapinzani hawawezi kujifunza kwa makosa yao kwa vipindi viwili hivi basi msemo wa Mh. Ndasa utaendelea kutamalaki. Kwamba mgombea wa kumshinda bado hajazaliwa katika jimbo la Sumve, na kama chama kikiendelea kumwamini ataliongoza jimbo hilo kwa awamu nyingine nyingi zaidi.

Udhabidhabina, unafiki, na umimi mwingi umetawala kwenye vyama vya upinzani kiasi cha kushindwa kuheshimu taratibu wanazojiwekea na kuzisimamia haswa. Viongozi wengi kwenye chama wanamini wakigombea nafasi ndani ya chama mathalani kukiwakilisha chama kwenye ngazi flani(udiwani, ubunge) baadhi hutumia mabavu hata kama wamezidiwa na kujipitisha.

Hii ilitokea kwenye jimbo la Kwimba ambapo mgombea/mshindi wa 3(inasemekana ni mwenyekiti wa chama wilaya) kwanza hakusaini matokeo kukubaliana na pia akasimama yeye kwenye ngazi ya ubunge na kuachwa nafasi ya pili(katibu wa chama mkoa) na ya kwanza(mwanachama wa kawaida) bila sababu za kueleweka. Licha ya mshindi wa kwanza kuwaacha kwa mbali wenzake.

Pamoja na yote, kuna mengi ya kujifunza zaidi katika siasa hizi za ubabe. Hata CCM pia mgombea mmojawapo kwenye kura za maoni jimbo la Sumve hakulidhika na yale matokeo na kupelekea kuhama chama(kwenda CUF). Kule akapata nafasi ya kugombea ngazi ya ubunge na kuchuana na mpinzani wake(ambaye aliamini hakushinda kwa halali kwenye kura za maoni).

Pengine chama cha mapinduzi kingejilaumu sana endapo huyo mgombea aliyekihama angeshinda kupitia upinzani kwenye nafasi hiyo.

Panapo majaliwa mbunge wa Sumve, katika kuhakikisha unawatumikia wananchi wako kama ulivyowaahidi. Na Usisahau hoja yako ya kugawa wilaya iwe na halmashauri mbili kuifuatilia kwa ukaribu zaidi ili kuboresha maendeleo yetu kwa kusogeza huduma karibu na wananchi.

Tafakari!
nguduone@gmail.com.



Sunday, May 1, 2016

AFISA MTENDAJI KATA YA MWAKILYAMBITI MATATANI KWA KUOMBA RUSHWA




















TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Mwanza, tarehe 21/04/2016 imemfikisha mahakamani Afisa Mtendaji wa kata ya Mwakilyambiti wilaya ya Kwimba BW. BONAVENTURA LUPILYA MAKUNGU(46) kwa kosa la kuomba hongo ya shilingi laki tatu (300,000/=) na kufanikiwa kupokea  shilingi (190,000/=) kutoka kwa JOHN MASHOMALI LUKUNGU(45).
Afisa mtendaji huyo aliomba pesa hiyo ili aweze kumpatia dhamana ndugu wa bwana 
JOHN MASHOMALI LUKUNGU(45), Bi  LUCIA SOBOLA JANELA ambaye yeye kama mlezi alikamatwa  kwa  kosa la utoro wa mwanafunzi LUCIA  MABULA JOHN.
Mtuhumiwa BW. BONAVENTURA LUPILYA MAKUNGU alitenda kosa hilo la kuomba na kupokea hongo mnamo tarehe 26/02/2016 ambapo ni kinyume na kifungu cha 15(1a) cha sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Namba 11/2007.
Mashtaka hayo yamefunguliwa katika Mahakama ya Wilaya ya Kwimba na Mwendesha Mashitaka wa TAKUKURU Bw. JOVINE  MAJURA ambapo yamesajiliwa kwa shauri la jinai namba 39/2016  na liko mbele ya Mheshimiwa Hakimu BONAVENTURA LEMA.
Akisomewa shauri hilo mbele ya Hakimu, Mtuhumiwa  BW. BONAVENTURA LUPILYA MAKUNGU(46) alikana shtaka hilo na yuko nje kwa dhamana  hadi shauri hilo litakapotajwa tena tarehe 24 Mei, 2016.
Wakati huohuo TAKUKURU Mkoa wa Mwanza pia inatarajia kumfikisha mahakamani Afisa Afya  na Mazingira Bw. SOSPETER JACOB SELEWA (29) wa kata ya Buswelu iliyopo Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, kwa kosa la kuomba rushwa ya shilingi Laki 100,000/= kutoka kwa Bi. LYDIA JULIUS TAMBILIJA ambaye ni mmiliki wa kituo cha kulelea watoto kinachofahamika kwa jina la JITAMBUE.
Afisa Afya huyo  aliomba pesa hiyo ili aweze kufungua kituo hicho cha  kulelea watoto ambacho awali alikifunga kwa vile kituo hicho hakikuwa na baadhi ya sifa zinazostahili.


Imetolewa Tarehe 22/042016 na ERNEST MAKALE, Mkuu wa TAKUKURU(M) 
Previous Page Next Page Home