Monday, May 23, 2016

STORI YA MAISHA YA NG'WANAMALUNDI-1


(Chanzo: gazeti la mwananchi, jan 2014)

Bottom of Form
Kwa Watanzania wenye umri mkubwa waliopata kusoma historia au kusikia hadithi za makabila, hasa ya Wasukuma na Wanyamwezi, hawakukosa kusikia habari ya Ng’wanamalundi.
Mtu huyo aliyewahi kuutingisha utawala wa Wajerumani, alizaliwa katika ukoo wa kawaida akiwa mcheza ngoma mashuhuri, mwaka wa kuzaliwa kwake haufahamiki ila alifariki dunia mwaka 1936, akiwa tayari mtu mzima.
Watu wengi wamekuwa wakimjadili kwa maoni tofauti, wengine wakimsifu kama shujaa huku wengine wakihusisha uwezo wake na nguvu za giza.
Katika makala hii usahihi wa historia yake unaelezwa na mjukuu wake wa pili, Kishosha Sitta (80) mkazi wa Kijiji cha Mwalugulu wilayani Kahama mkoani Shinyanga, anayesimulia alivyomfahamu babu yake huyo.
Sitta anaanza kueleza kuwa jina halisi la babu yake halikuwa Ng’wanamalundi bali lilikuwa Igulu Bugomola, ambaye alizaliwa katika Kijiji cha Mwakubunga Nera wilayani Kwimba mkoani Mwanza.
Ng’wanamalundi alikuwa mtoto pekee wa kiume na wa mwisho kati ya wanne, kwa baba yake Bugomola na mama yake, Ngolo Igulu.
Sitta anasema Igulu (Ng’wanamalundi), alikuwa na tabia ya uzururaji tangu utotoni na mara nyingi haikuwa rahisi kumkuta nyumbani. Alikuwa mashuhuri kutokana na umahiri wake wa kucheza ngoma na mara nyingi alipokuwa akitembea mitaani alifuatwa na kundi kubwa la watoto.
“Hali hiyo iliwachukiza wazazi wengi wenye watoto waliokuwa wakiambatana naye, kiasi cha kumchukia hata Ng’wanamalundi mwenyewe, kutokana na watoto wengi hasa waliokuwa wakitoka familia za wafugaji kutoweka na hiki kilikuwa chanzo cha mifugo mingi kupotea baada ya kutelekezwa na watoto hao,” anasema Sitta.
Hali ya kuchukiwa kwa Ng’wanamalundi ilienea pale kijijini kiasi cha kuanza kumkebehi, hasa kutokana na umbo lake refu na miguu yake myembamba kuanzia magotini hadi kwenye makanyagio, ikiwa mirefu kuliko kawaida.
Sitta anasema hali hiyo ilisababisha kumdhihaki na kumwongezea chuki zaidi kwa wanakijiji wa eneo hilo waliodiriki kumtukana kwa lugha ya Kisukuma; “Mamirundi galyo lilihumbura bana bise” ikiwa na maana ‘mamiguu yake marefu linarubuni watoto wetu”.
Hapo ndipo ukawa mwanzo wa kufutika kwa jina la Igulu na kuwa Ng’wanamalundi, jina ambalo lilitokana na urefu wa miguu yake na kila kona walimuita hivyo.
Kadiri siku zilivyosonga mbele Ng’wanamalundi alizidi kujiimarisha katika kikundi chake cha ngoma ambayo ilivuta vijana wengi, pia baadaye ilitumika kama jeshi la kukodiwa na Watemi inapotokea vita.
Pamoja na wazazi kumchukia sana, lakini vijana walimpenda na kikundi chake kikubwa cha ngoma kilipendwa na kutumika katika sherehe mbalimbali kwenye familia za Kitemi za wakati huo.
Mwanzo wa miujiza
Sitta anasema Ng’wanamalundi na wenzake wawili walikwenda kwa bibi kizee mmoja kutafuta dawa itakayowasaidia katika shughuli zao za kucheza ngoma, ambapo bibi kizee huyo alikubali kuwasaidia.
“Tujagi lolo ngh’wiporu bana bane akiwa na maana kwamba twendeni sasa porini watoto wangu. Mwanamalundi aliongozana na wenzake pamoja na kizee huyo mpaka porini.
“Walipofika porini bibi Kizee huyo alikamata vinyonga watatu na kuwaekea vichwani, kwa kila mmoja na kuendelea kusonga mbele porini, baada ya kufika katikati ya pori nene, kizee aliwaambia wote wasimame,” anasimulia Sitta.
Anasema baada ya kusimama aliamuru kila mmoja achimbe shimo lenye urefu hadi kiunoni, na baada ya kukamilika kwa mashimo hayo aliwaambia wakusanye kuni na kuzitumbukiza.
Baada ya kazi hiyo kukamilika Sitta anasema walipekecha moto na kuziwasha zile kuni na moto uliposhika kasi aliwachukua wale vinyonga watatu na kuwawekea dawa mdomoni na kisha aliwatupia ndani ya moto huo, wakateketea wote.
“Ng’wanamalundi na wenzake wakiwa bado wanashangaa vinyonga hao kuungua, ghafla alitokea kifaru kwenye moto huo na kuanza kuwakimbiza hovyo na wote wakasambaritika na bibi kizee wao,” anasema na kuongeza;
Ngw’anamalundi alikimbia akapanda juu ya mti, kifaru alifika kwenye shina la mti na kuanza kuliparua kwa hasira na baadaye aliondoka kabla hajafika mbali alimuona yule bibi kizee akikutana na faru huyo.”
Anasema Ng’wanamalundi alishuhudia kifaru akimrarua rarua bibi kizee mpaka akafa, kisha kifaru alitoweka kusikojulikana huku akimuacha Ng’wanamalundi asijue la kufanya juu ya mti.
Sitta anasema: “Ng’wanamalundi baada ya muda alishuka juu ya mti na kwenda kwenye maiti ya yule bibi kizee, akaamua aibebe mgongoni airejeshe nyumbani, lakini kabla hajafika mbali alisikia sauti ikisema, “Igulu bajahe abiyo akiwa na maana Igulu wenzako wamekwenda wapi”.
Sauti hiyo ilimshtua Ng’wanamalundi ambaye alimshusha bibi kizee mgongoni mwake na akashangaa kumuona akiwa hai asiyekuwa na jeraha lolote, kama alivyokuwa baada ya kushambuliwa na faru.
“Igulu tujage ahante ugo waliwalinaga, akiwa na maana Igulu twende kwenye mti uliokuwa umepanda, Ng’wanamalundi aliongozana na bibi kizee huyo mpaka kwenye ule mti aliyachukua magamba ya mti yaliyokuwa yameparuliwa na faru,” anasema Sitta.
Baada ya zoezi hilo kukamilika bibi kizee huyo alimtengenezea dawa aliyokuwa akihitaji, na kisha Mwanamalundi alirejea kwao kuendelea na shughuli zake za ngoma aina ya Kahena, ambayo mpaka leo inaendelea kwa jina lingine la Wigashe.
Anakutana na Mtemi Chlya
Sitta anaongeza kuwa, Ng’wanamalundi akiwa katika harakati zake za kujiimarisha katika masuala ya dawa zake za ngoma, alienda kuchimba kwenye pori la Mwandutu huko wilayani Maswa sasa ni Wilaya ya Kishapu, ambalo lilikuwa katika miliki ya Mtemi Chalya.
Imeelezwa kuwa baada ya kufika katika pori hilo akiwa na wafuasi wake wakiendelea kuchimba dawa, ghafla alitokea Mtemi Chalya na kumuuliza; “Ubebe nani wakuwilaga kwiza ngh’wiporu lyane” akiwa na maana; “Wewe nani amekuambia kuja kwenye pori langu?”
Mwanamalundi alimjibu; “ Ubebe ulintemi wa banhu pye nu nene nding’wenekele wa maporu pyee.” Akiwa na maana “Wewe ni Mtemi wa watu wote na mimi ni mmiliki wa mapori yote”. Kauli hiyo ilimuudhi Mtemi Chalya.
Anasema, kufuatia kauli hiyo Mtemi Chalya aliita jeshi lake kwa lengo la kuja kumkamata, lakini walishangaa baada ya kufika katika eneo waliloelezwa na Mtemi wao kuwa Ng’wanamalundi anatakiwa kukamatwa na kuuawa, lakini walishindwa baada ya kukuta simba wengi sana.
Jeshi hilo na Mtemi ilibidi kukimbia kujiokoa kwani simba hao walianza kuwashambulia, wengine walitawanyika ovyo na baadhi yao wachache tu ndiyo walionusurika.
Lakini cha kushangaza walipofika walimkuta Ng’wanamalundi na wafuasi wake wakimalizia kula chakula nyumbani kwa Mtemi Chalya, ambaye hata yeye alichanganyikiwa na kushindwa kuongea lolote.
Sitta anasema, Ng’wanamalundi baada ya kumaliza kula chakula kwa Mtemi Chalya aliondoka na wafuasi wake na akapitia kwenye lile pori akachimba dawa zake na kuondoka kwenda kuendelea na maisha yake.
“Katika ngoma zake; Ng’wanamalundi alikuwa na tabia ya kuwatahadharisha mashabiki wake kuacha kwenda wakiwa wamejipaka dawa yoyote ile, anasema. Aliwaambia: “Bing’we akwiziza munho wibilaga bugota bosebose ulu kutora akotora henaha,ulo nsabo akupandika heneha.”
Kauli hiyo ilikuwa na maana nyie asije mtu amejipaka dawa yoyote hapa kama ni kuoa, ataoa hapahapa kama ni mali atapata hapahapa, hata hivyo kuna wale walipuuza kauli hiyo kwa kuja wamejipaka dawa kwa lengo la kujipima uwezo wa dawa zao. Lakini hawakufanikiwa na badala yake walikufa.

inaendelea sehemu ya pili.....

No comments:

Post a Comment

Previous Page Next Page Home