Sunday, August 14, 2016

KWIMBA TUITAKAYO ITAPATIKANA KWA USHIRIKI MZURI WA WANANCHI NA VIONGOZI


(Hizi ni salamu zangu kwenu viongozi na wananchi wa Kwimba katika awamu hii ya HAPA KAZI TU)
BY NGUDU NYUMBANI BLOG
14/08/2016

Ni imani yangu kuwa wote tu wazima wa afya, tunaendelea na ujenzi wa taifa letu. Leo NGUDU NYUMBANI ingependa kuwakaribisha rasmi viongozi mbalimbali waliopewa majukumu mazito kuiongoza wilaya yetu kongwe ya KWIMBA katika awamu hii ya 5.
Bila shaka wengi wetu tunawafahamu viongozi wetu kuanzia ngazi ya vijiji, vitongoji, mitaa, kata, tarafa na hadi ngazi ya wilaya.

Kwa faida ya wengine ambao hawajui, Mkuu wa wilaya(DC) ya Kwimba kwa sasa ni  Mhandisi Mtemi Msafiri Simeon, Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya(DED) ni Pendo Anangisye Malabeja na Katibu tawala wa wilaya(DAS) ni  Andrea Izziga Ng’hwani. DED si mgeni kwetu sababu amewahi kuhudumu katika nafasi hiyo kabla.

Kuhusu wabunge wa majimbo ya Kwimba na Sumve bila shaka tunawajua, madiwani wetu na viongozi wengine wote wa ngazi zote tunawafahamu.

Awamu ya tano imeingia na kasi ya aina yake katika kuhakikisha inatoa majibu ya changamoto zinazowakabili wananchi wake, ikiongozwa vema na Rais wa JMT, Dr John Pombe Magufuli.

Katika mambo ambayo Rais  amekuwa akisisitiza kufanyiwa kazi na viongozi aliowateua katika ngazi mbalimbali hasa ngazi ya halmashauri za wilaya(mkurugenzi, Mkuu wa wilaya na Katibu tawala n.k) ni pamoja na;

Usuluhishaji wa migogoro ya ardhi  baina ya wakulima na wafugaji au wakulima dhidi ya mwekezaji au viongozi wa serikali na wananchi. Mfano mzuri ni mwezi wa pili mwaka huu pale Naibu waziri wa Ardhi, Nyumba na Maelndeleo ya Makazi Angelina Mabula alipombana Afisa ardhi wa wilaya ampatie maelezo kuhusu idara hiyo kuchukua fedha ya wananchi bila ya kuwagawia viwanja. Hayo na mengine mengi yanapaswa kupatiwa majawabu ya kudumu.

Tatizo la elimu hasa upungufu wa madawati ambalo kwa kiasi kikubwa limeshughulikiwa. Nilisoma taarifa moja ikimnukuu mkurugenzi wa wilaya akisema wilaya ya Kwimba ina nakisi ya madawati 5,314 sawa na asilimia 15 kumaliza tatizo la uhaba kufikia julai 30 mwaka huu. Hayo aliyazungumza wakati wa hafla fupi ya kupokea msaada wa madawati 60 yenye thamani ya Sh milioni 5 iliyofanyika shule ya msingi Kakora Kata ya Ngudu Mjini, kutoka kwa uongozi wa Benki ya CRDB tawi la Nyerere jijini Mwanza. Hivyo hadi kufikia julai 21 kulikuwa na upungufu wa madawati 5,254.

Maagizo mengine ya Rais ni pamoja na kukabiliana na baa la njaa pamoja na milipuko ya magonjwa katika mikoa na wilaya zote nchini.
Pia kupitia maagizo ya RC Mongella ya june 04 mwaka huu alipokuwa akiwaapisha  wakuu wa wilaya,  ambapo pamoja na yote alisisitiza wakasimamie shughuli za kuhimiza maendeleo, suala la ulinzi na usalama huku akitilia mkazo ukomeshwaji wa mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi na vikongwe.

Katika kuwakaribisha huko NGUDU NYUMBANI ingependa kuwakumbusha machache yaliyopo ndani ya wilaya yetu.

ELIMU
Pamoja na kukabiliana na tatizo la madawati, zoezi lililofanikiwa kwa kiasi kikubwa. Wilaya yetu bado ipo nyuma sana katika suala la elimu. Ningependa kulielezea hili kwa kuhusianisha na matokeo ya vijana wetu kwenye shule za msingi na sekondari.
Bahati nzuri teknolojia imekua kiasi hata cha matokeo ya upimaji wa kitaifa darasa la nne(SFNA), Matokeo ya darasa la saba, ya kidato cha pili yote yanawekwa kwenye mtandao. Ukipitia blogu yetu utayaona na kukubaliana nami.

Tatizo ni kubwa sana katika ufaulu wa shule zetu, mathalani vijana wanaohitimu kidato cha nne. Niliandika makala yenye jina ‘IDADI YA WALIOCHAGULIWA KIDATO CHA TANO KWA KILA SHULE ZILIZOPO WILAYA YA KWIMBA’ pia NGUDU NYUMBANI ilifanya tathmini ya matokeo ya kidato cha 4 mwaka 2015. Kwa waliofuatilia matokeo kwa ujumla au walau kusoma tathmini wanaweza kukubaliana nami kuwa bado tuna safari ndefu katika elimu yetu.

Shule za A-level zilizopo wilaya ya Kwimba walau zinafanya vizuri katika matokeo yao. Ambapo katika matokeo ya mwaka huu,  Mwamashimba H/school wameshika nafasi ya 2/25 kimkoa(ina division 1-3, hakuna four na zero), Sumve ikishika nafasi ya 11/25 kimkoa na Ngudu H/school nafasi ya 12/25 Kimkoa.

Mbali na matokeo, bado sekta ya elimu ina changamoto lukuki, ikiwemo uhaba wa nyumba za walimu, madarasa, uhaba wa walimu n.k.  ‘Elimu ni walimu’ kauli hii imewahi kutolewa maelezo jadidi na mujarabu na Prof  Kitila Mkumbo katika moja ya makala zake kwenye gazeti la Raia mwema, pia wadau wengine wamepata kusisistiza kauli hii. Bila kuwekeza katika changamoto zinazowakabili waalimu bado elimu yetu itabaki nyuma daima dawamu.

Pamoja na yote hayo wilaya yetu inaburuza mkia katika ufaulu kimkoa kwa muda sasa. Hivyo viongozi wenye dhamana ya kusimamia sekta hii wasifanye kazi kwa mazoea tungependa kuona mabadiliko.

KILIMO NA HALI YA UCHUMI
MWANZA ni miongoni mwa mikoa(mitano) inayoongoza kwa umaskini Tanzania na asilimia ya umaskini(35.3 %) hii ni kulingana na mpango wa maendeleo wa Taifa kwa mwaka wa fedha 2016/167.

kupitia gazeti la mwananchi waliandika kwamba, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi Dr, Tibeza alisema taarifa alizonazo zinatofautiana na alizopewa zinaonyesha kuwa Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa mikoa mitano inayokabiliwa na upungufu wa chakula.
Alinukuliwa akisema  “Taarifa nilizopewa na mthamini wa chakula zinasema Mwanza ni miongoni mwa (mikoa) inayokabiliwa na upungufu wa chakula, hivyo itakuwa na njaa, lakini wewe (Mongella-Mkuu wa Mkoa wa Mwanza) unaniambia kuna chakula cha kutosha,”.

Pamoja na yote hayo,asilimia kubwa ya wakazi wa Kwimba ni wakulima na wafugaji. wakulima  wanaotegemea zaidi mvua za masika ambazo mara nyingi hazieleweki na sio za kutegemea sana katika kilimo chao.

Mazao kama pamba, alizeti, mpunga, mahindi n.k ndiyo huliwa na wakulima japo ni kwa uchache ambao wengi wengi wao hulima kukidhi mahitaji ya familia na wachache hutegemea kuuza kujipatia kipato. 
Changamoto zilizopo hasa kwenye zao la pamba mikoa ya kanda ya ziwa ni nyingi na hazijapata ufumbuzi wa kudumu. Licha ya kuwa vinu kadhaa vya kuchambulia pamba bado zao hili halimnufaishi ipasavyo mkulima.

Bwawa la mahiga maalumu kwa kilimo cha umwagiliaji na uvuvi, kunapaswa kuwepo mipango mizuri katika kulitumia bwawa hili ili liweze kuwanufaisha wananchi na serikali kwa ujumla.
Elimu inapaswa kutolewa kwa wakulima, hasa kulima mazao yenye kuhimili ukame, utumiaji bora wa zana bora za kilimo n.k

UKUAJI WA TEKNOLOJIA
Ukuaji wa sekta ya teknolojia ya habari na mawasiliano kwa miaka ya hivi karibuni, imekuwa ikikua kwa kasi ukilinganisha na uhitaji wa watumiaji wa huduma zihusianazo na sekta hiyo. Kumekuwa na uwekezaji mkubwa katika hili, hali ambayo inatia moyo japo sio kwa kiwango kinachotakiwa lakini walau inaridhisha. 
Ukuaji wa TEHAMA umesababisha mabadiliko ya uendeshaji wa shughuli za serikali na jamii kwa ujumla.
Ukuaji wa sekta hii unahusisha na vitu vingi ambapo baadhi ni kama matumizi bora, sahihi na salama ya vifaa na mifumo ya TEHAMA  serikalini. Mbali na hilo pia, lengo jingine kubwa ni kurahisisha upatikanaji wa habari, uhuru wa kupata habari na kusambaza kwa wengine bila kuathiri, kuingilia, kukiuka au kuvunja katiba na sheria zote za nchi zinazolinda uhuru huo.  

Kwa leo nitaongelea zaidi kuhusu matumizi bora na sahihi ya vyombo vya Tehama hasa kwenye matumizi ya mitandao na intaneti(tovuti, barua pepe n.k)

Kuna uhitaji mkubwa kwa taasisi ama za serikali au binafsi kuwa na tovuti katika hatua mojawapo ya kurahisisha upatikanaji wa mambo muhimu yahusuyo taasisi husika. Hasa nikiongelea upande wa serikali, mamlaka zake nyingi zinatunza na kutoa taarifa zao kwenye tovuti. Ofisi ya Rais, na ofisi nyingine nyingi kubwa zinafanya hivyo pia.

Ni utaratibu mzuri unaokubalika katika kukuza secta ya TEHAMA, ambapo unarahisisha upatikanaji wa habari muhimu kwa wale wenye uwezo wa kutumia mitandao na intaneti kwa ujumla.
Ombi langu kwa hawa viongozi wetu ni kuhakikisha wilaya inakuwa na tovuti rasmi ambapo, habari zote muhimu za wilaya yetu zenye kupaswa kuwafikia wananchi ziweke kupatikana kule.

Sambamba na uanzishwaji wa hiyo tovuti, itasaidia viongozi waandamizi wa serikali ngazi ya wilaya kutumia barua pepe za serikali.

Mwongozo wa matumizi bora, sahihi na salama ya vifaa na mifumo ya Teknolojia ya habari na mawasiliano(TEHAMA) serikalini toleo la julai 2012, umesisitiza matumizi wa anwani za barua pepe hasa usajiri wa barua pepe za serikali.

 Anwani za barua pepe binafasi mfano  ‘yahoo.com’, ‘hotmail.com’, ‘gmail.com’ n.k hazipaswi kutumika katika mawasiliano ya shughuli za serikali.

Sasa sijui viongozi wetu wanatumia anwani zipi maana inaelekezwa taasisi za serikali anwani za barua pepe zao ziwe zenye kikoa cha mfumo wa ‘.go.tz’ na mfumo wa kifupisho cha cheo jina la taasisi na kikoa husika. Mfano anwani ya barua pepe ya mkurugenzi inaweza kuwa.. md@kwimbadc.go.tz na sio dedkwimba@yahoo.com iliyokuwa inatumika kabla.

Hiyo kwimbadc.go.tz  ndio tovuti inayopaswa iwepo hewani kwa maana ya kupatikana muda wote(umiliki wa domain name).

Kuna shida katika tovuti ya mkoa(www.mwanza.go.tz) hasa katika viungo(links) za wilaya, waliopata kutembelea tovuti hii wanaweza jua ninachomaanisha.

Mfano ukifungua kwenye link ya ‘Kwimba DC’ utafunguliwa ukurasa ukiwa wazi na ujumbe ukisema ‘Ukurasa huu upo kwenye matengenezo’  ni zaidi ya miaka miwili na zaidi sasa, enewei pengine matengenezo yanahitaji mwongo mzima tuendelee kusubiri.
Pamoja na hayo yote, kuna blogu moja(www.kwimbadc.blogspot.com) inayoripoti baadhi ya taarifa za halmashauri, japo sina hakika kama ndiyo inayotambulika. Kupitia blogu hiyo kuna ‘jarida la Kwimba’ toleo la 45 lenye jina ‘IJUE KWIMBA’.
 Kwa ambao hamjapata kusoma ni vema mkapitia kuna mambo mazuri ya kuyajua mule japo kwa ufupi. Pia kuna Documentary ya miaka 10 ya maendeleo ya KWIMBA 2005-2015.

Ningependa kumaliza kwa leo, kwa kunukuu baadhi ya maneno kwenye kitabu cha Uhuru na Maendeleo kilichoandikwa na Baba wa Taifa hayati Mwl J.K Nyerere, alisema;

Kama maendeleo yanaongeza uhuru wa watu, basi lazima yawe maendeleo yanayowafaidia watu. Lazima maendeleo hayo yawe na faida kwao, na kumaliza shida zao. kila mpango uamuliwe kwa kupima kama unatimiza shabaha ya maendeleo, na shabaha ya maendeleo ni  watu. Lakini kama mpango unasaidia maendeleo ya watu na kama unatimizwa na watu kwa hiari yao, mpango huo utatimiza haja za watu, mradi masharti matatu yametimizwa. Kwanza, kama watu wanaelewa shida zao. Pili, kama wanaelewa jinsi shida hizo zinavyoweza kumalizwa. Na tatu, kama wana uhuru wa kujiamulia mipango yao, na kuitimiza.

Itaendelea……

Tafakari!

nguduone@gmail.com

No comments:

Post a Comment

Previous Page Next Page Home