Thursday, January 1, 2015

TAARIFA KUHUSIANA NA MTOTO MWENYE ULEMAVU WA NGOZI ALIYETEKWA HUKO TARAFA YA MWAMASHIMBA WILAYANI KWIMBA.


Jeshi la polisi mkoani mwanza linawashikilia watu wanne, akiwemo baba mzazi, Emmanuel shirinde(28) wa mtoto mwenye ulemavu wa ngozi, pendo emmanuel ambaye aliporwa na watu wasiojulikana waliovamia nyumbani kwao

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, Valentino Mlowola, tukio la uporwaji wa mtoto huyo lilitokea Desemba 27, mwaka huu saa 4.30 usiku katika kijiji cha Ndami tarafa ya Mwamashimba wilayani Kwimba mkoani hapa.

Akifafanua, Kamanda Mlowola alisema siku ya tukio saa 4.30 usiku Shirinde akiwa amelala nyumbani kwake na familia yake, akiwemo Pendo, walivamiwa na watu wawili wasiojulikana.
 

Alisema watu hao walivunja mlango kwa kutumia jiwe kubwa, maarufu kama ‘fatuma’, ambapo waliingia ndani na kumchukua mtoto huyo huku wakimzuia baba mtu kupiga kelele.

Kamanda Mlowola alisema baba wa mtoto, alisema baada ya mtoto wake kuporwa, alisikia mlio wa pikipiki ikiondoka nyuma ya nyumba yake na ndipo alipotoa taarifa Polisi, ambao walifika eneo la tukio saa 7 usiku.

Alisema kwa kuwa kijiji wanachoishi kipo mpakani mwa wilaya ya Misungwi na Kwimba, polisi wa wilaya hizo walishirikiana kuwasaka bila mafanikio.

Hata hivyo, alisema timu ya Polisi kutoka makao makuu, imewasili ili kusaidiana na polisi wa mkoani hapa kumsaka mtoto huyo ili apatikane akiwa hai.

“Tunamshikilia baba mzazi ili aweze kutusaidia, mazingira ya kijiji sio rahisi watu kutoka mbali wakafahamu kama nyumba fulani ina mtu mwenye ulemavu wa ngozi, lazima waliongozwa na mwanakijiji,” alisema Kamanda.

Kutokana na tukio hilo, Jeshi la Polisi limeahidi kutoa zawadi ya Sh milioni tatu kwa mtu yeyote atakayetoa taarifa zitakazowezesha kupatikana kwa mtoto huyo.

Hili ni tukio la kwanza la kuporwa kwa mtu mwenye ulemavu wa ngozi mkoani hapa, kuripotiwa tangu mwaka huu uanze na kwamba ni tukio la nne nchini.

Kamanda Mlowola alitoa rai kwa wananchi wa mkoa wa Mwanza, wenye taarifa juu mtoto huyo washirikiane na Jeshi la Polisi ili kuokoa maisha ya mtoto huyo.

Takwimu zilizotolewa na Chama cha Albino Tanzania (TAS) wakati wa maadhimisho ya Siku ya Amani Kimataifa, zinaonesha kuwa kutoka mwaka 2006 hadi Septemba 2014, albino 74 wameshauawa kikatili, huku 56 wakinusurika kifo na 11 kati yao wameongezewa ulemavu mwingine wa kudumu.


No comments:

Post a Comment

Previous Page Next Page Home